2015-01-05 07:59:34

Taizè kuwasha moto wa Injili mjini Valencia 2016


Vijana wa Jumuiya ya Kiekumene ya Taizè kutoka nchi mbali mbali za Ulaya, waliokuwa wanakusanyika mjini Prague, nchini Czech, ili kusali, kutafakari na kushirikishana imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, mwishoni mwaka 2015 watakusanyika Jimbo kuu la Valencia, nchini Hispania, ili kuwasha moto wa Injili ya Kristo; tangazo ambalo limepokelewa kwa mikono miwili na Familia ya Mungu, Jimbo kuu la Valencia.

Kardinali Antonio Canizares wa Jimbo kuu la Valencia, Hispania anawaalika vijana wa Jumuiya ya Kiekumene ya Taizè kuanza kujinoa tayari kushiriki kikamilifu katika mkutano wao wa thelathini na nane, utakaofanyika Jimboni mwake. Hii itakuwa ni nafasi ya kukutana na kusali kwa ajili ya kuombea umoja wa Kanisa, ili kutekeleza amri ya Kristo, ili wote wawe wamoja, ili walimwengu wapate kuamini na kwa kuamini waweze kuwa na matumaini mapya!

Umati mkubwa wa vijana umeshiriki katika mkutano wa thelathini na saba uliokuwa unafanyika mjini Prague, kiasi cha kuwashangaza watu waliokutana nao. Hawa ni vijana waliokuwa wanatema cheche za furaha, imani na matumaini, huku wakionesha heshima kwa watu na mazingira.

Vijana wanaoamini na wale wasioamini, walijikuta wakishiriki katika sala na tafakari, zaidi hata na matarajio ya wale waliokuwa wameandaa tukio hili la Kikanisa. Vijana hawa ambao walipata hifadhi kwenye familia na taasisi mbali mbali mjini Pargue, walikuwa wanakusanyika kwenye Makanisa makuu kumi na saba mjini humo.

Fra Alois ametangaza kwamba, mwezi Aprili 2015, akiwa ameambatana na umati wa vijana wa Jumuiya ya Kiekumene ya Taizè, wanatarajiwa kwenda mjini Moscow, Russia, ili kuhudhuria Siku kuu ya Pasaka ya Waorthodox, ili kuonesha umuhimu wa kushikamana kwa pamoja, ili walimwengu wapate kuamini!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.