2015-01-03 12:21:08

Askofu mkuu atishiwa maisha, huko Bangui!


Askofu mkuu Dieudonnè Nzapalainga wa Jimbo kuu la Bangui, Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati, hivi karibuni alitishiwa maisha, makazi yake kuchomwa moto hivi karibuni baada ya kutembelea kambi ya wakimbizi kutokana na mchafuko ya kisiasa yanayoendelea nchini humo.

Kikundi kinachopingana na Kikosi cha balaka kilimtishia maisha, lakini hajukali kitu kwani anasema, ni kheri Kiongozi kujisadaka maisha yake, ili kweli: haki, amani, upendo na mshikamano viweze kupatikana. Vijana wanaotumiwa na baadhi ya wanasiasa ni kundi linalohitaji majiundo na mshikamano wa kweli, ili kusimama kidete kulinda na kutetea amani, badala ya kuwa ni vibaraka wa wanasiasa wachache wanaowatumia kwa ajili ya mafao yao binafsi!

Askofu mkuu Nzapalainga anawataka waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutubu na kumwongokea Mwenyezi Mungu, kwa kuonesha upendo na mshikamano kwa watu walioguswa na kutikiswa na vita pamoja na migogoro na kinzani zinazoendelea nchini humo. Watu wanataka kujenga maisha yao kwa kujikita katika matumaini, utu na heshima ya binadamu.

Kanisa linapenda kumwilisha mafundisho yake kwa njia ya huduma ya mapendo kwa Mungu na jirani, ndiyo maana, kuna haja kwa watu ambao wanaendelea kutishia maisha ya watu kuweka silaha zao chini, huku wakiongozwa na dhamiri zao nyofu, kuona shida na mateso ya wananchi wengi wasiokuwa na hatia. Wananchi wa Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati wanapaswa kushirikiana, ili kuanzisha mchakato wa ujenzi mpya wa nchi yao, kwa kuendeleza pia upatanisho, msamaha, haki na amani.

Katika mapambano ya silaha kati ya Seleka na Balaka, zaidi ya watu elfu mbili wamepoteza maisha yao, na kuna kundi kubwa la watu ambalo limeyakimbia makazi yake kwa kuhofia usalama wa maisha yake. Katika mazingira kama haya, Kanisa limeendelea kutoa msaada kwa wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi maalum bila ubaguzi, kwani linatambua kwamba, wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, wanapaswa kupendwa, kuthaminiwa na kuhudumiwa kadiri ya uwezo uliopo!







All the contents on this site are copyrighted ©.