2015-01-02 11:35:10

Jengeni amani inayosimikwa katika udugu!


Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu sanjari na maadhimisho ya Siku ya 48 ya Kuombea Amani Duniani, ni matukio ambayo yanapaswa kuwaongoza waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, wanatoa kipaumbele cha pekee kwa uwepo wa Yesu Kristo kati yao, ili aendelee kuwaangaza na kuwakirimia neema na baraka katika mapito ya maisha yao ya kila siku!

Yesu Mwana wa Mungu aliyezaliwa ni zawadi inayoonesha kwamba, Mungu anaokoa, changamoto na mwaliko kwa waamini kujikita katika hija ya toba na wongofu wa ndani, kama chachu ya kukua na kukomaa katika maisha ya kiroho na kiutu; tayari kujenga na kuimarisha umoja, upendo na mshikamano wa kidugu, kwa kutambua kwamba, wote ni ndugu na hakuna tena mtumwa, kwani wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Katika utu na heshima ya binadamu, Makanisa yanapaswa kuonesha umoja na mshikamano kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko.

Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Kardinali Angelo Scola, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Milano, lililoko nchini Italia, tarehe Mosi, Januari 2015 ambaye amekazia pamoja na mambo mengine umuhimu wa kujenga na kudumisha udugu ambao ni kielelezo makini cha uhuru wa mtu binafsi. Pale dhambi inapobomoa na kuharibu mahusiano kati ya Mungu na mwanadamu, ubinafsi unachukua na nafasi na hapo ni mwanzo wa mifumo mbali mbali ya utumwa.

Kardinali Scola anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kujikita katika mchakato wa ujenzi wa misingi ya haki, amani na maridhiano; kwa kuondokana kabisa na misimamo mikali ya kiimani ambayo imekuwa ni Njia ya Msalaba kwa Wakristo huko Mashariki ya Kati. Ni watu ambao wamejaribiwa sana na vita, dhuluma na nyanyaso, wana woga na kweli wamechoka sana kutokana na mateso na mahangaiko ya kila siku, lakini imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, bado ni hai na inawawezesha kushinda woga, mchoko na hali ya kukata tamaa.

Kardinali Scola anawaalika waamini kuendelea kuwa ni wajenzi wa amani inayojikita katika ukweli, haki, upendo na uhuru wa kweli kama alivyokazia Mtakatifu Yohane XXIII, ili kujenga dunia mpya, kwa kufanya mabadiliko ya kweli katika taasisi na mashirika ya kimataifa yaliyopo, ili kukidhi mahitaji msingi ya binadamu katika ulimwengu mamboleo.

Maadhimisho ya Siku ya Kuombea Amani Duniani, uwe ni mwanzo wa maandalizi ya maadhimisho ya Fumbo la Pasaka, yaani, mateso, kifo na ufufuko wa Kristo, utimilifu wa Fumbo la Umwilisho, linalopania kumwokoa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.