2015-01-01 09:20:44

Siku ya Yohane Paulo II nchini Canada 2015


Serikali ya Canada kwa kutambua mchango wa Mtakatifu Yohane Paulo II katika kulinda, kutetea na kudumisha misingi ya haki, amani, utu na heshima ya binadamu, imepitisha sheria inayoanzisha Maadhimisho ya Siku ya Yohane Paulo II, ambayo itaadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 2 Aprili, siku aliyofariki dunia, Baba Mtakatifu Yohane Paulo II.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linaipongneza Serikali kwa hatua hii muhimu ambayo inatambua na kuthamini mchango wa Mtakatifu Yohane Paulo II katika kukuza na kuendeleza uhuru, utu na heshima ya binadamu. Kwa mara ya kwanza siku hii inaadhimishwa tarehe 2 Aprili 2015, miaka kumi, tangu Papa Yohane Paulo II alipofariki dunia.

Sheria hii mpya iliyotungwa nchini Canada inatambua mchango na dhamana iliyotekelezwa na Mtakatifu Yohane Paulo II katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Alisaidia sana mchakato wa majadiliano, haki na amani kati ya watu wa mataifa. Ni kiongozi aliyekuwa na mvuto wa pekee kwa vijana, kiasi cha kuwahamasisha vijana hao kuambatana na Yesu Kristo katika maisha yao, kwa kumwilisha mafundisho yake katika uhalisia wa maisha yao.

Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu Yohane Paulo II alitembelea nchini Canada mara tatu; katika mwaka 1984, 1987 na mwaka 2002. Ni kiongozi aliyebahatika kutembelea nchi mbali mbali duniani, kiasi hata cha kuchangia kuporomoka kwa Ukomunisti, Ulaya ya Mashariki.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.