2014-12-31 11:43:08

Jamani, tegeni sikio msikilize kile anachosema Papa Francisko!


Juhudi zinazofanywa na Baba Mtakatifu Francisko katika kulinda, kutetea na kuendeleza utu na heshima ya binadamu; haki na amani; ustawi na maendeleo ya wengi zinapaswa kuungwa mkono na watu wote wenye mapenzi mema sehemu mbali mbali za dunia, lakini kwa namna ya pekee na wananchi wa Ufilippini ambao wanasubiri kwa hamu kubwa, ujio wa Baba Mtakatifu Francisko nchini mwao!

Ni mwaliko maalum unaotolewa na Alhaji Ebra M. Moxsir, Kiongozi mkuu wa Baraza la Maimamu wa dini ya Kiislam nchini Ufilippini anayewaalika ndugu zake Waislam pamoja na watu wenye mapenzi mema, kumsikiliza kwa makini ushauri unaotolewa na Baba Mtakatifu Francisko ili kushinda vitendo vya kigaidi, kwa kujenga na kuendeleza majadiliano ya kidini, ili kupata amani ya kweli na inayodumu.

Alhaji Moxsir ameyasema haya katika mahojiano maalum na Kituo kimoja cha Televisheni nchini Ufilippini, kwa kukazia mahusiano mema ya kidini miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali, mahusiano yanayojikita katika misingi ya: ukweli, uwazi, upendo, mshikamano na mafao ya wengi. Kuna haja ya kuondokana na misimamo mikali ya kiimani inayohatarisha usalama na maisha ya watu na hivyo kuwa kikwazo kikuu cha maendeleo na ustawi wa watu. Waamini wafundishwe kanuni msingi za imani yao, ili kuishuhudia katika uhalisia wa maisha ya kila siku. Misimamo mikali ya kidini ni matokeo ya waamini kutofundwa kikamilifu katika misingi ya imani na kanuni maadili.

Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kufanya hija yake ya kichungaji Barani Asia kuanzia tarehe 12 hadi tarehe 19 Januari 2015. Akiwa nchini Ufilippini, Baba Mtakatifu atakutana na kuzungumza na wahanga wa tufani ya Yolanda, iliyopelekea maafa makubwa kwa watu na mali zao. Anatarajiwa pia ukutana na kuzungumza na viongozi wa kidini, ili kuimarisha mchakato wa majadiliano ya kidini na kiekumene, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya watu: kiroho na kimwili.

Kwa maneno mengine, hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Ufilippini inapania kuwatia moyo waamini ili kujikita zaidi katika mchakato wa kupambana na umaskini kwa njia ya huduma inayosimikwa katika upendo na huruma! Vijana wengi kutoka Ufilippini wanaendelea kujiandaa ili kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko, ili aweze kuwatia shime katika mchakato wa Uinjilishaji mpya. Tukio la vijana kukutana na Baba Mtakatifu Francisko, litapambwa kwa sala, tafakari na Ibada ya Rozari Takatifu. Vijana wanatarajiwa kutoa ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake!







All the contents on this site are copyrighted ©.