2014-12-30 11:15:43

Vijana jengeni mshikamano wa kimataifa!


Bwana Ban Ki-Moon, Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anawapongeza vijana kutoka katika nchi mbali mbali za Bara la Ulaya wanaokutanika mjini Prague, Jamhuri ya Watu wa Czech, kwa ajili ya kushiriki katika mkutano wa thelathini na saba wa Vijana wa Jumuiya ya Kiekumene ya Taizè, changamoto kwa vijana sehemu mbali mbali za dunia kuhakikisha kwamba, wanajikita katika ujenzi wa umoja na mshikamano kwa kushinda kishawishi cha utaifa, sera na ubaguzi; mambo amabyo yanawagawa watu.

Wakati huu ambapo dunia inateseka kutokana na vita na kinzani mbalimbali, kuna haja ya kuwa na vijana wanaokutana na watu mbali mbali, ili kuanza tena mchakato wa upatanisho unaopania pamoja na mambo mengine, kudumisha amani na usalama, chachu ya maendeleo endelevu itakayowasaidia vijana kutumia vipaji na karama zao kwa ajili ya mafao ya wengi. Kuna haja ya kushirikiana ili Jumuiya ya Kimataifa iweze kufaidika na mawazo na mikakati ya maisha, kwa kuwajibika zaidi na hatimaye, kuona matunda ya kazi zao.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anawataka vijana kujikita katika mikakati ya maendeleo endelevu, wakati huu Jumuiya ya Kimataifa inapoangalia kwa matumaini mkutano wa kimataifa wa mabadiliko ya tabianchi unaotarajiwa kufanyika huko Paris Ufaransa, kunako mwaka 2015. Lengo ni kuweka mikakati ya kupunguza kiwango cha nyuzi joto ili kufikia walau sentigrade mbili, ili kuepuka athari za mabadiliko ya tabianchi.

Vijana wanapaswa kuwa ni wadau wakuu katika mchakato huu unaolenga kujikita katika maendeleo endelevu. Huu ni wajibu fungamanishi unaojikita katika mshikamano, ili kujenga misingi ya amani, kwa kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu; mahali ambapo utawala wa sheria unaheshimwa!

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anawatia shime vijana kuonesha vipaumbele katika maisha yao mintafafu: amani, maendeleo na haki msingi za binadamu. Vijana wanahamasishwa kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika maisha ya kijamii, kwa kutoa maoni na kuyatekeleza, ili kujenga dunia iliyo bora zaidi. Umoja wa Mataifa utaendelea kuwaunga mkono vijana katika mikakati kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.