Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, tarehe 21 Machi 2015 anatarajiwa kufanya hija
ya siku moja kwenye Madhabahu ya Bikira Maria wa Pompei, yaliyoko kwenye Jimbo kuu
la Napoli, Kusini mwa Italia. Taarifa hii imetolewa na Askofu mkuu Tommaso Caputo
na kuthibitishwa na Idara ya Habari ya Vatican. Baba Mtakatifu anatarajiwa kwenda
huko ili kusali kwa Bikira Maria wa Rozari Takatifu, anayeheshimiwa sana nchini Italia.
Ibada kwa Bikira Maria imekuwa ni chemchemi na kichocheo kikuu cha waamini
kuonesha mshikamano a upendo na huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni
mwa jamii. Uwepo wa Baba Mtakatifu Francisko, ni tukio muhimu sana katika mchakato
wa kuwaimarisha ndugu zake katika Kristo ili waendelee kujisadaka kwa ajili ya ustawi
na mafao ya maskini na wanyonge ndani ya jamii!
Hija hii pamoja na mambo mengine
anasema Askofu mkuu Caputo inapania kukazia upendo, haki, utu na heshima ya binadamu,
aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Baba Mtakatifu anatarajiwa kuwaonesha dira
na mwelekeo wa kuendelea kumwilisha imani katika matendo, kwa njia ya huduma.
Itakumbukwa
kwamba, kunako tarehe 21 Oktoba 1979, Mtakatifu Yohane Paulo II alitembelea Jimbo
kuu la Napoli na kwenye Madhabahu ya Pompei na baadaye alirejea tena kwenye Madhabahu
haya kunako tarehe 7 Oktoba 2003, ili kufunga Mwaka wa Rozari Takatifu. tarehe 19
Oktoba 2008, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI alitembelea Madhabahu haya.