Baba Mtakatifu Francisko amewashukuru na kuwapongeza wanachama wa Chama cha Umoja
wa Wanafamilia wengi nchini Italia, waliofika mjini Vatican kutoka mjini Brescia,
alikozaliwa Mwenyeheri Papa Paulo VI, ili kusherehekea pamoja Siku kuu ya Familia
Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, Jumapili tarehe 28 Desemba 2014. Wao ni kielelezo
kwamba, familia hizi zinapenda kulinda na kutangaza Injili ya Uhai.
Baba Mtakatifu
katika hotuba yake, amewaambia kwamba, Familia ni kielelezo tosha cha watu kutaka
kukutana na kusaidiana kwa hali na mali. Familia hizi zimefika mjini Vatican zikiwa
zimesheheni zawadi ya ubaba na umama inayopokea na kukumbatia uhai. Ikumbukwe kwamba,
watoto ni zawadi maalum katika historia ya maisha; ni kundi linaloleta mabadiliko
ya mfumo na mtindo wa maisha ya familia. Watoto ni maajabu ya Mungu yanayochochea
mabadiliko ya kina; ni matunda ya upendo kati ya Baba na Mama, wanaokuwa na kukomaa
katika upendo.
Watoto wanaotoka kwenye familia za watu wengi, wana uwezo wa
kujenga udugu na mshikamano tangu wakiwa watoto wadogo tofauti kabisa na ubinafsi
unaoendelea kuwameza watu wengi kwa nyakati hizi. Familia zenye watoto wengi ni shule
ya mshikamano na umoja, tunu msingi katika maisha ya kijamii. Watoto ni matunda ya
familia yenye mizizi yake kutoka kwa wazee. Familia ya binadamu ni sawa na msitu mkubwa
unaozaa matunda ya mshikamano, umoja, imani, msaada, usalama, kiasi, furaha na urafiki.
Ni kielelezo cha matumaini ya jamii, kwa kusaidiana na kurithishana imani, maadili
na utu wema.
Baba Mtakatifu Francisko anakiri kwamba, wazee wengi Barani Ulaya
wamekuwa ni chachu ya imani kwa wajukuu wao, kwani wamewasaidia kupata imani kwa njia
ya Sakramenti ya Ubatizo pamoja na kuendelea kuwarithisha imani, matumaini na mapendo
katika hija ya maisha yao.
Baba Mtakatifu anawapongeza wazazi kwa kupenda na
kuthamini zawadi ya Uhai tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake
hadi mauti ya kawaida inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu. Hii ni dhamana nyeti inayotekelezwa
katika mazingira magumu na wakati mwingine pasi na msaada kutoka Serikalini, hata
kama kuna sera na mikakati ya kusaidia familia zenye watu wengi, lakini sera hizi
zimebaki katika maneno tu.
Baba Mtakatifu Francisko anachukua fursa hii kuwahamasisha
wanasiasa na watunga sera nchini Italia kuhakikisha kwamba, wanaunga mkono juhudi
za familia hizi, kwani kila familia ni chanzo cha jamii husika, lakini familia zenye
watoto wengi zina utajiri mkubwa kwa jamii, kumbe, Serikali inapaswa kutoa kipaumbele
cha kwanza kwa kuwekeza kwenye familia kama hizi, ili ziweze kutekeleza dhamana na
wajibu wake barabara.
Baba Mtakatifu anavihamasisha vyama na mashirika ya kitume
yanayojikita katika familia, kujitokeza na kushiriki kikamilifu katika medani za kisiasa
na kijamii ili waweze kuchangia katika utungaji wa sera na mikakati kwa ajili ya familia,
kwa kutetea na kulinda tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Vyama hivi vya kitume
vijitokeze hata katika maisha na utume wa Kanisa mahalia.
Baba Mtakatifu anasema,
ataendelea kuwasindikiza katika sala na maombi yake na anapenda kuwaweka chini ya
ulinzi, usimamizi na tunza ya Familia Takatifu ya Nazareti. Anawashukuru na kuwapongeza
kwa kujenga nyumba mjini Nazareti kwa ajili ya familia kutoka sehemu mbali mbali za
dunia zinazokwenda kufanya hija katika Nchi Takatifu.
Baba Mtakatifu anaendelea
kuziombea familia ambazo zimeathirika kutokana na myumbo wa uchumi kimataifa, kwa
kukosa fursa za ajira; familia zinazokabiliana na na matatizo pamoja na changamoto
mbali mbali za maisha, kamwe zisikate tamaa na hatimaye, kutumbukia katika upweke
hasi, kinzani na migawanyiko. Kila mtu aweze ni kielelezo cha upole na faraja kutoka
kwa Mwenyezi Mungu.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili
ya Radio Vatican.