Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia katika maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 tangu
Zambia ilipojipatia uhuru wake wa bendera, lilikazia kwa namna ya pekee, umuhimu wa
wananchi wa Zambia kujikita katika kujenga na kudumisha misingi ya haki na amani;
ukweli na umoja; udugu na usawa; daima wakitafuta mafao ya wengi. Zambia kwa sasa
inajiandaa kwa ajili ya uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika hapo tarehe 20 Januari
2015 kufuatia kifo cha Rais Michael Chilufya Sata.
Tangu wakati huo, vyama
vya kisiasa vimejikita katika kampeni ya kuomba ridhaa kutoka kwa wananchi, jambo
ambalo mwanzoni lilianza kutishia amani, usalama na mustakabali wa taifa la Zambia.
Wachunguzi wa mambo wanasema, watu wamesherehekea Noeli huku kampeni za uchaguzi mdogo
zikiendelea kupamba moto!
Changamoto kubwa kwa sasa nchini Zambia ni mwendelezo
wa umoja na mshikamano wa kitaifa uliojionesha katika kipindi cha miaka hamsini iliyopita,
licha ya wananchi wa Zambia kusigana kwa maneno, lakini bado wameendelea kuwa wamoja,
licha ya cheche za ufisadi kuanza kuchomoza wakati wa kampeni kwa kuoneshana ubabe
wa fedha. Wanasiasa hawana budi kujifunga kibwebwe ili kuhakikisha kwamba, wanasaidia
kupambana na umaskini wa hali na kipato nchini Zambia, kwa kutumia rasilimali iliyopo
kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi. Hadi sasa kumekuwepo na malalamiko kwamba,
utajiri na rasilimali ya nchi havijagawanywa sawa miongoni mwa wananchi wote!