2014-12-26 08:18:05

Uzuri na utakatifu wa Familia!


Askofu mkuu Carlos Osoro Sierra wa Jimbo kuu la Madrid, Hispania katika barua yake ya kichungaji kwa ajili ya maadhimisho ya Siku kuu ya Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kufanya tafakari ya kina ili kuona uzuri na ukweli wa familia, mambo msingi yanayojikita katika moyo wa kila mwanadamu. Itakumbukwa kwamba, Siku kuu ya Familia Takatifu inaadhimishwa tarehe 28 Desemba 2014. RealAudioMP3

Familia kama Kanisa dogo la nyumbani, mahali ambapo umoja na mshikamano katika maisha vinapaswa kuwa ni sehemu ya vinasaba vyake; ni mahali ambapo zawadi ya uaminifu na udumifu katika maisha ya ndoa na familia inachipuka na kuchukua sura yake katika maisha ya wanandoa. Familia inaimarishwa kwa uwepo wa upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo, mwamba wa tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.

Familia zikijijenga na kujisimika katika mwamba ambao ni Yesu Kristo, kamwe hazitaweza kuyumbishwa katika maisha na utume wake. Kutokana na ukweli huu, Injili ya Familia itaendelea kuwa ni Habari Njema kwa ajili ya ulimwengu na chemchemi ya furaha kwa wengi, licha ya kinzani na changamoto nyingi zinazoikumba familia kwa nyakati hizi.

Askofu mkuu Osoro anaialika Familia ya Mungu Jimboni mwake, kuhakikisha kwamba, inaadhimisha Siku kuu ya Familia Takatifu, kwa kuzionjesha familia zenye shida na mahangaiko makubwa, ile furaha, imani, matumaini, mapendo na mshikamano wa dhati. Bado kuna familia ambazo zimeathirika vibaya sana kutokana na myumbo wa uchumi kimataifa, hizi ni familia ambazo zinapaswa kuonjeshwa umoja, mshikamano na upendo.

Askofu mkuu Osoro anazikumbusha familia umuhimu wa kushiriki kikamilifu katika maisha ya Kisakrakenti kwa kupokea mara kwa mara Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na Kitubio, ili kweli Yesu aweze kupata nafasi katika maisha yao ya kila siku. Anawaalika wanandoa watarajiwa kuhakikisha kwamba, wanajiandaa kikamilifu kwa ajili ya kukumbatia na kuenzi tunu msingi za maisha ya ndoa na familia, tayari kusaidiana katika hija ya maisha ili kufikia utakatifu na maisha ya uzima wa milele, lengo kuu katika maisha ya Wakristo.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.