Watanzania wanaaswa kukitumia Kipindi cha Noeli kwa kuhakikisha kwamba wanadumisha
amani, upendo na mshikamano na kamwe wasikubali, watu wachache wasiokuwa na nia njema
na taifa wawagawe kwa misingi yoyote ile. Kauli hiyo imetolewa katika mkesha wa Sikukuu
ya Noeli na Askofu mstaafu Mathias Isuja Josefu wa Jimbo Katoliki Dodoma wakati akiongoza
Ibada ya Misa Takatifu katika Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo wa msalaba, Jimboni Dodoma.
Askofu
Isuja amewataka Wakristo na watu wote wenye mapenzi mema kusherekea Sikukuu ya Noeli
kwa kudumisha upendo na amani kwani hata Yesu Kristo alikuja duniani kwa ajili ya
kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti na kumkirimia: furaha,
amani na matumaini mapya.
Amesema kuwa sikukuu ya Noeli iwaunganisha watu
wawe pamoja, washirikiane katika mambo yote lakini kwa namna ya pekee, kwa kuwasaidia
masikini na wenye shida zaidi. Watanzania wametakiwa kuwa makini na utandawazi usiojali
utu, heshima, upendo na mshikamano, kwani unaweza kuwatumbukiza katika majanga makubwa
ya maisha. Baadhi ya watu katika jamii, wameathirika kutoka na utandawazi kwa kujiingiza
katika biashara haramu ya binadamu, utumwa mamboleo, misimamo mikali ya kiimani; mambo
ambayo yanahatarisha amani, ustawi na mustakabali wa Jumuiya ya Kimataifa.
Wakati
huohuo Padre Dominiki Mwaluko akiongoza Ibada ya sikukuu ya Noeli katika Kigango cha
Mtakatifu Maria de Mathias, kilichoko Jimbo Katoliki la Dodoma, amewataka Wakristo
wawe ni watu wenye msimamo thabiti katika misingi ya imani, matumaini na mapendo,
kwa kuendelea kuwa ni chachu ya amanim, utulivu na mshikamano unaofumbatwa kutoka
katika undani wa maisha yao. Wakristo wawe ni chachu ya maisha adili na matakatifu,
kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao. Waamini wajitahidi kujisadaka kwa ajili ya Mungu
na jirani zao, kwa kuachana na dhambi pamoja na nafasi zake.
Aidha kwa upande
wa Parokia ya Kiwanja cha Ndege Jimbo Katoliki la Dodoma ambalo hivi karibuni limepandishwa
hadhi na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Jimbo kuu, jumla ya watoto 120 wamebatizwa
katika Siku kuu ya Noeli.
Katika mahubiri yake, Padre Sostenes Luyembe,
SJ, amewataka wazazi kuendelea kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai,
kwa kuhakikisha kwamba, wanawarithisha watoto wao imani, maadili na utu wema, daima
wakionesha shukrani kwa Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya watoto. Ujumbe wa Noeli anasema
Padre Luyumbe unaopaswa kujikita katika mioyo na maisha ya watu ni kwamba, nyumba
ya Kristo ni haki, amani na mapendo; nguzo msingi katika kuitegemeza familia ya mwanadamu.
Kwa
upande wa waamini wa Parokia ya Bikira Maria Mama wa Damu Azizi ya Yesu, Kisasa Medelii,
Jimbo Katoliki la Dodoma, Padre Parfect Leiya amewataka waamini kutumia Kipindi cha
Noeli, ili kumwilisha upendo kwa Mungu na jirani zao, lakini zaidi kwa kuwajali maskini
na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.
Padre Leiya, Paroko wa Parokia
hii amesema Noeli ni Sikukuu ya Familia inayojikita katika furaha, imani, matumaini,
mapendo, huruma na faraja kwa kutoa nafasi ya pekee ili Yesu Mfalme wa amani na mshauri
wa ajabu aweze kupata makao katika familia, ili kuziimarisha ziweze kuwa kweli ni
shule ya utakatifu, haki, amani, msamaha na upatanisho, wakati huu Mama Kanisa anapojitahidi
kutangaza Injili ya Familia kwa walimwengu!
Padre Leiya amewataka waamini
na watu wote wenye mapenzi mema, kutubu na kumwongokea Mungu kwa kutembea katika mwanga
angavu unaoletwa na Mtoto Yesu. Ni mwaliko wa kuachana na matendo ya giza na kuambatana
na Yesu, ambaye ni ukweli, njia na uzima.
Katika Kikanisa cha Kijiji cha
Matumaini, Jimbo Katoliki Dodoma, kinachowahudumia watoto wanaoishi na virusi vya
Ukimwi; Padre Vincenti Boselli, muasisi wa Kijiji hiki katika mahubiri yake wakati
wa kuadhimisha Siku kuu ya Mtakatifu Stefano Shahidi, inayoadhimishwa na Mama Kanisa
kila mwaka ifikapo tarehe 26 Desemba, amewataka waamini kushuhudia imani, kuiadhimisha,
kuimwilisha katika matendo adili na kuisali, kama kielelezo cha ushuhuda wa imani
tendaji; imani ambayo Mtakatifu Stefano iliishuhudia hata mbele ya watesi wake, akawa
tayari kujisadaka kwa ajili ya sifa na utukufu wa Kristo.
Mtakatifu Stefano
aliitetea imani yake kwa matendo, akawa tayari kutoa msamaha hata kwa watesi wake,
akifuata mfano wa Yesu mwenyewe aliyefundisha umuhimu wa msamaha hata alipokuwa ametundikwa
pale juu Msalabani. Noeli, iwe ni Siku kuu ya kuonjeshana: huruma, upendo na msamaha
kutoka kwa Mwenyezi Mungu, kwani kwa njia ya Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, Mungu
ameingia katika historia ya maisha ya mwanadamu, ili kumkomboa kutoka katika dhambi
na mauti, tayari kumshirikisha maisha ya uzima wa milele.
Zawadi kubwa wanayopaswa
kuwaonjesha na kuwashirikisha wengine ni upendo, msamaha, imani na matumaini wale
wote waliokata tamaa katika maisha yao, kwani Kristo aliyezaliwa ni sababu ya furaha,
imani na matumaini.