2014-12-26 08:11:18

Furaha ya Injili ya Familia!


Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kutoka kifua mbele ili kuwatangazia na kuwashirikisha walimwengu furaha ya Injili ya Familia, Mama Kanisa anapoadhimisha Siku kuu ya Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, inayoadhimishwa tarehe 28 Desemba 2014. RealAudioMP3

Maaskofu wanaitaka Familia ya Mungu nchini Hispania kujifunga kibwebwe ili kuinjilisha na kutangaza Injili ya Familia, kwa kuwa na mwelekeo sahihi kuhusu utu na heshima ya binadamu; upendo na tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Hii ni changamoto kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kutambua upendo wa kweli unaojionesha kama wito mtakatifu kutoka kwa Mwenyezi Mungu na wala si katika kuridhisha tamaa na vionjo vya mwili; mambo ambayo wakati mwingine yanaacha ukakasi, majuto na machungu katika maisha ya mwanadamu.

Wito wa upendo kati ya Bwana na Bibi unapata utimilifu wake katika moyo wa mwanadamu, kwa kujikita katika uhuru na furaha ya kweli inayobubujika kutoka katika undani wa wapendanao. Wito wa upendo ni kiini cha Injili ya Familia wanasema Maaskofu wa Hispania na ndilo chimbuko la upendo wa Mungu unaomwilishwa katika maisha ya mwanadamu.

Huu ni upendo unaopania kuendeleza Injili ya Uhai katika maisha ya mwanadamu mintarafu mshikamano wa upendo kati ya Bwana na Bibi na wala si vinginevyo. Maaskofu wanasema kwamba, ilimpendeza Mwenyezi Mungu kuchagua fadhila ya upendo kama njia ya kumshirikisha Bwana na Bibi katika kuendeleza kazi ya uumbaji. Kumbe, upendo, uaminifu na udumifu kati ya Bwana na Bibi ni kielelezo cha upendo na uaminifu wa Kristo kwa Mchumba wake, yaani Kanisa.

Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linasema kwamba, dhamana na utume wa wazazi katika malezi na makuzi ndani ya familia hauna mbadala. Wazazi wanawajibu wa kuwafundisha na kuwarithisha watoto wao ukweli kuhusu tunu msingi za maisha ya kifamilia; na taasisi za Kiserikali hazina budi kusaidia mchakato huu kwa kutunza, kulinda na kuendeleza taasisi ya familia, kwa kutambua kwamba, Familia inawajibu pamoja na mambo mengine kuhakikisha kwamba, inarithisha imani hai inayomwilishwa katika uhalisia wa wanafamilia wote, ili kukuza na kuimarisha: furaha, upendo na matumaini.

Kanisa, kama Jumuiya ya Waamini linakumbushwa kwamba, linawajibu mkubwa wa kuendeleza mchakato wa Uinjilishaji, kwani wamepokea na kuonjeshwa upendo wa Mungu, unaowawajibisha kuwa ni mashuhuda wa upendo mpya ili uweze kuwa ni chachu inayochachua tamaduni katika ulimwengu mamboleo, ili watu waweze kusimama kidete kulinda na kutetea upendo wa kweli ambao ni asili ya Injili ya Uhai, kama msingi wa Jumuiya na maisha ya binadamu.

Mwishoni, Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linawaalika kwa namna ya pekee, Familia za Kikristo pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuonesha ushuhuda wa furaha ya Injili ya Familia katika nyumba zao, Parokia na Majimbo yao, kwa kuwashirikisha maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, furaha, upendo na matumaini mapya yanayobubujika kutoka katika Injili ya Familia!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.