Katika mkesha wa Noeli, Mama Kanisa anaadhimisha Siku kuu ya Kuzaliwa kwa Yesu Kristo,
Masiha na Mkombozi wa ulimwengu, anayekuja kumkomboa mwanadamu kutoka katika utumwa
wa dhambi na mauti; kutoka katika giza na kumwonesha mwanga wa maisha na matumaini
mapya. Utumwa kama ilivyokuwa kwa Waisraeli katika Agano la Kale, ni kielelezo cha
mateso, mahangaiko na hali ya kukata tamaa.
Kumbe, kuzaliwa kwa Yesu Kristo
kama ilivyotabiriwa na Manabii katika Agano la Kale ni ishara ya neema ya Mungu inayotaka
kumfunda mwanadamu kutenda mema na kuachana na uovu pamoja na mabaya katika maisha.
Kwa bahati mbaya, Kipindi cha Noeli kimevamiwa na kugeuzwa kuwa ni muda muafaka wa
biashara, kiasi cha kupoteza maana halisi ya Noeli ambayo kimsingi inapata chimbuko
lake katika mazingira ya kipagani, lakini, Kanisa likaitamadunisha na kuwa ni Siku
ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo Mkombozi wa dunia!
Noeli inayoadhimishwa tarehe
25 Desemba ya kila mwaka, ikapata mwelekeo wa pakee katika Fumbo la Umwilisho, pale
ambapo Neno wa Mungu alipotwaa mwili na kukaa kati ya binadamu na katika mambo yote
alikuwa sawa na binadamu, isipokuwa hakutenda dhambi. Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa
na Askofu Severine Niwemugizi wa Jimbo Katoliki Rulenge-Ngara wakati wa maadhimisho
ya Ibada ya Misa Takatifu, Kesha la Noeli, tarehe 24 Desemba 2014. Siku kuu hii bado
inapata upinzani kutoka kwa wapinga Kristo ambao hata pamoja na kujiita kuwa ni "Wakristo
bado imani yao inatia shaka: Fumbo la Umwilisho, Fumbo la Pasaka na Ekaristi takatifu".
Hawa ni watu ambao wanajizolea umaarufu mkubwa katika vyombo vya upashanaji
habari kwa kuyakita mahubiri yao katika miujiza: kulisha, kuponya na utajiri. Askofu
Niwemugizi anasema, tarehe si hoja, jambo linalopewa kipaumbele cha kwanza ni Fumbo
la Umwilisho!
Siku ile alipozaliwa Yesu, Malaika waliwapasha watu habari juu
ya tukio kuu katika historia ya maisha ya mwanadamu, wachungaji wakakimbia kwa haraka
kwenda kustaajabia matendo makuu ya Mungu na Mamajusi kutoka Mashariki wakafunga safari
kwenda kumwona na kumsujudia Masiha aliyezaliwa mjini Bethlehemu. Wachungaji walikuwa
ni maskini watu waliokuwa wanakabiliwa na changamoto mbali mbali za maisha kama ilivyo
kwa watu wa nyakati hizi.
Askofu Niwemugizi anasema, kuna watu wanateseka na
kuhangaika: kiroho na kimwili; hawana matumaini ya kesho iliyo bora zaidi kutokana
na magonjwa, ukosefu wa fursa za ajira, ukata, hofu, mashaka na wasiwasi. Kuna wafungwa
na mahabusu gerezani ambao hawajui hatima ya maisha yao, lini kesi zao zitasikilizwa
na haki kutendeka. Kuna waamini wana vifungo vya maisha ya kiroho kiasi kwamba, wanashindwa
kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa. Wote hawa wanahitaji ukombozi
na matumaini mapya yanayoletwa na Yesu Mkombozi wa ulimwengu!
Askofu Niwemugizi
anasema, hali ya amani na usalama nchini Tanzania kwa mwaka 2013, ilikuwa inatisha
kiasi cha kuwalazimisha waamini kusali mapema jioni, kwa kuhofia usalama wa maisha
na mali zao, lakini kwa sasa mambo yamebadilika, waamini wameweza kwenda kusali na
kushiriki kikamilifu katika kesha la Noeli kwa amani na utulivu, matendo makuu ya
Mungu. Hizi zote ni changamoto zinazohitaji kukombolewa.
Kuna baadhi ya waamini
hata katika Kipindi hiki cha Noeli, wanaendelea kushikwa na simanzi pamoja na huzuni
kwa kuondokewa na wapendwa wao; kwa kukosa nafasi ya kukutana na kumujuika na ndugu
na jamaa zao kutokana na sababu mbali mbali. Kuna watu ambao wanaandamwa na ukata,
kiasi kwamba, hawana uhakika wa maisha yao wakati huu wa Kipindi cha Noeli. Kuna watoto
ambao hawakubahatika kupata nguo mpya kwa ajili ya kusherehekea Noeli na Mwaka Mpya!
Askofu
Severine Niwemugizi anawakumbushwa waamini wote hawa kwamba, jambo la msingi ni kutambua
kwamba, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili anakuja kati yao, Yeye ni sababu ya furaha
na matumaini yao; ni chemchemi ya upendo, furaha, amani, utulivu na matumaini. Wakati
wa Majilio, waamini walihimizwa, kujenga moyo na utamaduni wa subira na matumaini,
kwa kumsubiri Yesu Mkombozi wa dunia, ili aweze kuzaliwa tena katika maisha yao. Ujio
wa Yesu, ambao kimsingi ni kielelezo cha imani, matumaini, mapendo, amani na mshikamano,
uwapatie mwelekeo mpya wa maisha.
Kwa njia ya Fumbo la Umwilisho linalopata
utimilifu wake katika Fumbo la Pasaka, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Yesu, mwanadamu
amekombolewa kutoka katika lindi la dhambi na mauti; hiki ni kiini cha imani inayotangazwa
na Mama Kanisa katika maisha na utume wake. Yesu ni neema ya Mungu inayosafisha, takasa
na kuokoa. Yesu ndiye Masiha, Mkombozi na Mpakwa wa Bwana wenye uwezo wa kifalme,
kikuhani na kinabii mabegani mwake.
Askofu Niwemugizi anasema, Noeli ni kipindi
cha kujisadaka, kujitoa na kujimega kwa ajili ya kuwashirikisha wengine ile furaha
ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo Mkombozi wa dunia. Ni kipindi cha kujikana, ili jirani
waweze kufaidika zaidi, kama ilivyokuwa kwa Yesu Kristo mwenyewe aliyeteseka, ili
kumkirimia mwanadamu furaha, matumaini na maisha ya uzima wa milele. Yesu Kristo ndiyo
sababu ya furaha ya kweli katika maisha ya mwanadamu.
Hii ni changamoto kwa
waamini kukumbatia Injili ya Maisha na kuachana kabisa na tabia ya kufumbata utamaduni
wa kifo unaosababisha machungu, simanzi na huzuni katika jamii. Hiki ni kishawishi
kibaya kinachopaswa kuepukwa. Wakristo wanapaswa wasiwe ni sababu ya huzuni kwa jirani
zao, kwa kujifunza kutokana na makosa, ili kutenda kwa kuwajibika zaidi. Uchaguzi
wa Serikali za mitaa uliofanyika nchini Tanzania katika siku za hivi karibuni, hakwenda
sawasawa, changamoto ya kujifunza kwa makosa kama haya, ili kufanya maboresho zaidi.
Maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, iwe ni sababu ya furaha kwa wengine!