2014-12-24 11:21:37

Salam za Noeli kwa Wananchi wa Korea kutoka kwa Papa Francisko!


Baba Mtakatifu Francisko amewatumia wananchi wa Korea ujumbe wa matashi mema wakati huu Mama Kanisa anapoadhimisha Siku kuu ya Noeli, huku akikumbuka kwa furaha na shukrani hija yake ya kitume aliyoifanya nchini humo, mwezi Agosti, mwaka huu.

Baba Mtakatifu anakumbuka kwa namna ya pekee, maadhimisho ya kukata shoka kwa ajili ya kuwakumbuka Mashahidi wa imani, mkutano wake na vijana kutoka sehemu mbali mbali za Bara la Asia na matukio mengine katika hija hii yataendelea kubaki kuwa ni kumbu kumbu ya kudumu katika maisha na utume wake.

Baba Mtakatifu anasali ili kwamba, mwanga angavu unaoiangazia dunia kutoka kwa Mtoto Yesu aliyezaliwa Bethlehemu, uijaze daima mioyo, familia na jumuiya zao. Noeli ni siku kuu ambayo Yesu anapenda kuwavuta watu kwake kwa njia ya wema wake wa kimungu. Yesu ni mwema, tena mwema sana anasema Baba Mtakatifu. Uwepo wake pekee unaweza kumkirimia mwanadamu furaha ya kweli, bila Yesu, hakuna jambo la maana, kwani Yesu ana nguvu ya kufanya yote mapya pamoja na kuwakirimia watu maisha mapya.

Mwishoni, Baba Mtakatifu anawaalika waamini na wananchi wote wa Korea kusali na kumwombea katika maisha na utume wake, wote anawatakia amani na utulivu katika kipindi hiki cha Noeli.







All the contents on this site are copyrighted ©.