Papa asema: huduma ni kukidhi hitaji linalolengwa.
Jumatatu, 21 Desemba 2014, nyakati za adhuhuri, Baba Mtakatifu alikutana na wafanyakazi
wa Vatican na Ofisi za Curia ya Roma, baada ya kukutana na Wakrugenzi na Maofisa wa
ngazi za juu wa Jimbo Takatifu na utawala wa Vatican. Madhumuni ya Mkutano huu ilikuwa
kutakiana heri za Siku Kuu ya Noeli.
Hotuba yake kwa wafanya kazi wote wa
Vatican iliongozwa na maneno ya Mtakatifu Augustino aliyesema ni majivuno yaliyomfanya
malaika kuwa ibilisi, na ni unyenyekevu unao wafanya watu kuwa sawa na malaika.
Baba
Mtakatifu Francisco, pamoja na kutoa shukurani kwa idadi kubwa ya wafanyakazi wazawa
wa Italia, pia kwa namna ya pekee aliwashukuru pia wafanyakazi kutoka mataifa ya
nje ya Italia , ambao kwa ukarimu wamejitoa katika huduma ya Kanisa , mbali na nchi
zao na familia zao , na hivyo kuwakilisha sura ya Kanisa moja la ulimwengu.
Kama
ilivyokuwa katika hotuba yake kwa Wakuu wa Idara za Curia ya Roma ,pia kwa wafanyakazi
wa kawaida, Papa alisisitiza umoja wa Kanisa kama ilivyo katika viungo vya mwili
wa mtu , ni vingi lakini vyote hufanya kazi kwa kushirikiana , na hivyo unakuwa ni
mfano mzuri hai kwa mwili wa Kristo ambalo ni Kanisa lake Takatifu. Kwa mtazamo huo
Papa aliwaalika wote, kuchunguza dhamiri na kutafakari vyema wakati huu wa kipindi
cha Noeli na mwaka mpya . Alihimiza kurejea katika sakramenti ya upatanisho kwa moyo
mnyenyekevu , na kumpokea kwa upendo Bwana anayebisha hodi katika mlango wa roho ,
kumpokea kwa furaha ya familia.
Papa aliwashukuru wote akisema kila mmoja
wao ana thamani kubwa katika utumishi wote, kama tu ulivyo mwili, kila kiungo, uwepo
wake ni muhimu. Na wao ni viungo katika mwili wa Curia ya Roma .
Papa aliendelea
kueleza kuwa huduma maana yake ni ufanikishaji wa lengo, ina maana kutazama kwa
makini, mahitaji ya anayehudumiwa, ina maana ya kukubali kutoa au kupokea huduma.
Papa aliwapa mfano wa mama anaye hudumia mtoto wake mgonjwa, mama huyo hujali katika
hali zote maumivu ya mwanawe. Yeye kamwe hatazami saa , wala kulalamika kutokana na
kutolala usiku wote, lakini anacho jali zaidi ni mtoto wake kuondokana na hali ya
maumivu hayo kwa gharama yoyote.
Kwa maneno hayo, Papa aliwasihi kukifanya
kipindi hiki cha Noeli kuwa wakati muafaka kwa ajili ya kuponya kila jeraha la uchungu
wa uhaba wa huduma na kupajaza kila palipo pungukiwa.
Alisema, huu ni wakati
wa kutibu maisha ya kiroho, na kujenga uhusiano wako na Mungu, kwa sababu huu ni
uti wa mgongo, kwa kila jambo tunalolifanya na kwa kila jinsi tulivyo. Mkristo ambaye
hajilishi kwa sala, sakramenti na Neno la Mungu, ni wazi hufifia na kunyauka na kufa.
Kutibu maisha ya kiroho, au kutibu maisha ya familia, kuwapa watoto na wapendwa
wengine si fedha tu, lakini wakati wote, huduma na upendo. Ni wakati wa kutibu
mahusiano na watu wengine , kuleta upya wa imani katika maisha na maneno na matendo
mema, hasa wale wanaohitaji zaidi. Ni wakati wa kutibu majadiliano, kusafisha lugha
na maneno yenye kukera, kuondokana na lugha ya matusi na kihuni. Ni kupona majeraha
ya moyo kwa mafuta ya msamaha, kuwasamehe wale waliotujeruhi kiroho na kuomba msamaha
kwa majeraha tuliyo sababisha kwa wengine.
Ni wakati wa kuhudumu kwa moyo
wenye shauku, unyenyekevu, ustadi, na hamu ya kujua jinsi ya kumshukuru Bwana, huu
ni wakati wa kutafuta kutibu dhidi ya moyo wa wivu, tamaa, chuki na hisia hasi zenye
kukumeza amani ya ndani na yenye kubadilisha watu kwa ndani na kuwa watu wa kuharibiwa
na uharibifu, ni wakati wa kutibu uchungu wenye kuleta moyo wa kisasi, na uvivu
ambayo unaongoza kwa katika hamu za kutaka msaada wa kuondosha maisha, kwa kuongozwa
na kiburi, na malalamiko ya mara kwa mara yanayoongozwa na kukata tamaa.
Papa
alieleza na kusema anazielewa hali hizi , ambazo hatima yake haiishii pazuri, bali
katika uharibifu .Na hivyo amemwomba Bwana , hekima iweze kuuongoza ulimi wakati
mazungumzo , si kusema maneno ya matusi, ambayo huacha uchungu kinywani.
Papa
ameomba wote kutafuta huduma ambamo Roho wa Krismasi , isigeuzwe kuwa Siku kuu
ya ulaji wa kibiashara , au utoaji wa zawadi zisizo kuwa na manufaa , lakini iwe ni
sikukuu ya furaha ya kumjongea Bwana katika pango la Noeli lililomo ndani ya moyo.
Papa
ameomba ili kwamba, Krismasi hii na iwe katika uhalisi wake wa kuwa Sikukuu ya umaskini
wa Mungu ambaye alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa (cf. Phil 2,6);
Mungu anayejiweka katika utumishi (Mat 22:27); Mungu aliyewaficha wenye hekima
na akili, na kuwafunulia walio wadogo na maskini (Mat 11:25); "Mwana wa Mtu hakuja
kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa maisha yake kuwa fidia ya wengi" (Marko 10:45).
Zaidi
ya yote , hii ni sikukuu ya Amani inayoletwa duniani na mtoto Yesu, "Amani kati
ya mbingu na nchi, amani miongoni mwa watu wote, amani katika mioyo yetu; amani kuimba
pamoja na na malaika: "Utukufu kwa Mungu juu na amani duniani kwa watu wenye mapenzi
mema" (Lk 2:14). Amani kama hitaji katika shauku zetu, katika huduma zetu, na katika
kutia joto katika moyo wenye baridi, yenye kuzihamasisha roho zilizopondeka kwa huzuni,
amani yenye kuangaza wepesi wa macho wepesi, katika kuuona mwanga wa uso Yesu! Kwa
amani hii, Papa alikamilisha na maneno ya kuwatakia kila la heri wafanyakazi wote
wa Vatican na familia zao, na pia aliomba msamaha kwa mapungufu yake mwenyewe binafsi
na kwa niaba ya kanisa , kwa baadhi ya kashfa zinazo sababisha madhara kwa Kanisa.
Aliwaomba pia wasisahau kumwombea.