2014-12-23 07:29:20

Kesha la Noeli, mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatano tarehe 24 Desemba, 2014, anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya mkesha wa Siku kuu ya Noeli, katika Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kuanzia saa 3: 30 Usiku kwa saa za Ulaya. Ibada hii ya Misa Takatifu itatanguliwa na wimbo wa Kalenda unaotangaza Fumbo la kuzaliwa kwa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, aliyetabiriwa na Manabii tangu Agano la Kale.

Yesu Kristo ni kielelezo cha Agano Jipya kati ya Mungu na mwanadamu, ili aweze kumkirimia tena amani na ustawi baada ya Waisraeli kutembea katika giza la maisha, katika utumwa na mahangaiko mbali mbali utumwani Misri, hatimaye wakakombolewa kwa mkono wenye nguvu kutoka kwa Mwenyezi Mungu, aliyekuwa anaambatana na Mtumishi wake mwaminifu Musa.

Kuzaliwa kwa Yesu Kristo Mkombozi wa dunia ni tukio ambalo linafumbatwa katika historia ya utawala wa Kirumi, uliokuwa chini ya Kaisari Oktaviani Augusto, wakati huo, amani ilikuwa inatawala katika uso wa dunia, Yesu Kristo, Mwana wa Baba wa Milele, aliyetungwa kwa uwezo wa Roho Mtakatifu kwake yeye Bikira Maria, akawa Mwanadamu na kuzaliwa mjini Bethlehemu. Kalenda ni wimbo wa sifa na utukufu kwa Yesu Kristo, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili!

Baba Mtakatifu Francisko, wakati wa Siku kuu ya Noeli, majira ya saa 6: 00 Mchana kwa Saa za Ulaya, anatarajiwa kutoa ujumbe wake wa Noeli kwa mji wa Roma na Dunia kwa ujumla na baadaye kutoa baraka yake ya kitume kama inavyojulikana kwa lugha ya Kilatini "Urbi et Orbi". Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican, itakuwa nawe bega kwa bega ili kukujuza yale yanayoendelea ndani na nje ya Vatican, wakati huu Mama Kanisa anaposherehekea Siku kuu ya Noeli.







All the contents on this site are copyrighted ©.