Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda yuko Doha, Qatar kwa ziara ya siku tatu kwa
mwaliko wa Serikali ya nchi hiyo. Lengo la ziara ya Waziri Mkuu ni kukuza mahusiano
baina ya nchi hizi mbili, kuangalia fursa za kiuchumi na miradi mikubwa inayoweza
kuzinufaisha nchi hizo na nje ya mipaka yake kwenye Ghuba ya Arabuni (Arabian Gulf)
na Bara la Afrika.
Vile vile Waziri Mkuu anatarajiwa kutangaza fursa za uwekezaji
nchini Tanzania, fursa za biashara, za utalii na kutafuta mitaji kwa ajili ya sekta
za uchimbaji gesi na mafuta, usindikaji mazao, uvuvi na mifugo, ajira na uendelezaji
miundombinu. Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano
wa Kimataifa, Waziri Mkuu atakuwa na mazungumzo ya kiserikali na Waziri Mkuu wa nchi
hiyo, Sheikh Abdulla Nasser Al Thani. Vilevile atakutana na Mawaziri wa Kazi na Ustawi
wa Jamii; Uchukuzi; Miundombinu na Uwekezaji wa nchi hii. Naibu Mawaziri atakaokutana
nao ni wa Uchumi na wa Nishati.
Vilevile Waziri Mkuu amepangiwa kukutana na
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara wa Qatar (Qatar Business Community), wajumbe
wa Chama cha Wafanyabiashara cha Qatar (Chamber of Commerce of the State of Qatar)
na pia atakutana na Watanzania waishio Qatar. Atatembelea pia Mamlaka ya Bandari ya
Qatar na makao makuu ya kampuni ya uchimbaji gesi ya Qatar.
Waziri Mkuu amefuatana
na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk. Titus Kimani; Waziri wa Kilimo na Maliasili
wa Zanzibar, Dk. Sira Ubwa Mamboya; Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa, Bw. Mahadhi Maalim; Naibu Waziri wa Nishati, Bw. Charles Kitwanga; Naibu
Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Bw. Godfrey Zambi. Wengine ni Mkuu wa Mkoa
wa Mbeya, Bw. Abbas Kandoro, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Bi. Halima Dendego, wabunge wawili
Bi. Amina Makilagi na Bw. Aeshy Hilali na Wakuu wa taasisi za TPSF na TPDC.