2014-12-22 11:40:15

Mfungulieni Kristo malango ya maisha yenu!


Padre Gabriel Mmassi, SJ. ni kati ya maelfu ya waamini na mahujaji waliofurika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kusali pamoja na Baba Mtakatifu Francisko, wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili tarehe 21 Desemba 2014. RealAudioMP3

Padre Mmassi anasema, kipindi cha Noeli ni wakati muafaka wa kumfungulia malango ya maisha Yesu anayezaliwa tena katika mioyo ya watu! Ni wakati wa kuendelea kukesha kwa sala na tafakari ya Neno la Mungu kama alivyofanya Bikira Maria, kiasi hata akathubutu kukubali Neno wa Mungu aweze kumwilishwa ndani mwake, na tangu hapo akawa kweli ni Tabernakulo ya Neno wa Mungu aliyefanyika mwili.

Majilio na hatimaye Kipindi cha Noeli ni wakati wa kuonjeshana upendo na mshikamano, amani na utulivu, kwani amani ni zawadi kubwa inayoletwa na Yesu Kriisto Mwana wa Mungu. Waamini na watu wote wenye mapenzi mema, waendelee kumwombea Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wake, ili aendelee kuwaongoza, kuwafundisha na kuwatakatifuza Watu wa Mungu kwa njia ya utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Baba Mtakatifu Francisko bado anaendelea kulihamasisha Kanisa kushikamana na maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii. Haya si mafundisho mapya bali ni mwendelezo wa agizo la Yesu Mwenyewe kwa wafuasi wake, kama yalivyomwilishwa na Wakristo wa Kanisa la Mwanzo. Kanisa linatambua kwamba, maskini ni hazina kubwa ya maisha na utume wa Kanisa!







All the contents on this site are copyrighted ©.