Noeli 2014: Wafanyakazi wa Vatican kukutana na Papa Francisko!
Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, ameamua kwa moyo
mkuu kukutana na kuzungumza na wafanyakazi wa Vatican pamoja na familia zao Jumatatu,
tarehe 22 Desemba 2014. Hili ni tukio la kihistoria, kwa kukumbuka kwamba, si rahisi
sana kwa wafanyakazi wa Vatican kuhudhuria katika matukio kama haya kwani mara nyingi
Baba Mtakatifu anapokuwa na shughuli, wao pia wanachakarika kuhakikisha kwamba, mambo
yanakwenda kama yalivyopangwa!
Kwa Mwaka huu, Baba Mtakatifu anataka kuzungumza
nao, ili kuimarisha moyo wa upendo na mshikamano katika familia kwa kutambua sadaka
na majitoleo yanayotolewa na wafanyakazi wa Vatican katika maisha na utume wa Kanisa.
Tukio la kutakiana kheri na matashi mema kwa Kipindi cha Noeli, linakuja wakati ambapo
Mama Kanisa anawahimiza wanafamilia kuendelea kutangaza Injili ya Familia kwa njia
ya ushuhuda wa maisha yao adili na matakatifu, ili kusaidia pia mchakato wa maadhimisho
ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya familia, itakayofanyika mjini Vatican kuanzia tarehe
4 hadi tarehe 25 Oktoba 2015.