Maskini ni hazina kubwa kwa Kanisa na binadamu katika ujumla wake!
Shirikisho la Jumuiya ya Yohane XXIII linatekeleza utume wake katika nchi 34 duniani
na Barani Afrika wako: Zambia, Tanzania, Kenya, Burundi na Cameroon. Ni shirikisho
linalowajumuisha Wakleri, Watawa na Waamini Walei, ili kushiriki kikamilifu katika
maisha na utume wa Kanisa, kwani linatambuliwa na Mama Kanisa katika jitihada za kuwahudumia
maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.
Shirikisho hili lilianzishwa
na Padre Oreste Benzi, ambaye hivi karibuni Jimbo Katoliki la Rimini Italia, limeanzisha
mchakato, ili aweze kuandikwa katika orodha ya majina ya Wenyeheri ndani ya Kanisa,
kwani anatambulikana sana kutokana na mchango wake wa huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa Jamii kama ambavyo aliwahi kusema Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI.
Ni
Shirikisho linalojibidisha kuwaendea na kuwahudumia maskini na wahitaji zaidi, kwa
kuwarudishia utu na heshima yao wanawake na wasichana waliokuwa wametumbukizwa katika
utumwa mamboleo pamoja na kuwahudumia maskini wanaojionesha kwa sura na kwa nyakati
tofauti.
Huu ni ushuhuda uliotolewa na Bwana Giovanni Paolo Ramonda, Mratibu
mkuu wa Shirikisho la Jumuiya ya Yohane XXIII walipokutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu
Francisko mjini Vatican siku ya Jumamosi, tarehe 20 Desemba 2014. Anasema, kuna idadi
kubwa ya vijana wanaotaka kukutana na Yesu katika umaskini na utupu wao; kuna maelfu
ya watu wanataka pia kujipatanisha na Mungu kwa njia ya Yesu Kristo; kwa hakika kuna
watu wanaotaka kukutana na Yesu kwa njia ya Kanisa linalowajali na kuwahudumia maskini
na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.
Shirikisho hili linapenda kuendelea
kubeba Msalaba kwa kusaidiana na maskini, kwa kuwashirikisha nguvu inayobubujika kutoka
katika Sakramenti ya Ekaristi Takatifu, Neno la Mungu na matendo ya huruma, kwa kutambua
kwamba, maskini na wanyonge ni hazina kubwa kwa Kanisa na binadamu katika ujumla wake.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio vatican