2014-12-19 16:30:30

Mti wa Noeli ni kielelezo cha mwanga, matumaini na mapendo!


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 19 Desemba 2014 amekutana na ujumbe kutoka Jimbo kuu la Verona na Catanzaro ili kuwashukuru kwa zawadi kubwa ya Mti wa Noeli ambao umepambwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican; mti ambao kwa sasa ni kivutio kikubwa kwa mahujaji na watalii wengi wanaoendelea kumiminika mjini Vatican kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Baba Mtakatifu anawashukuru viongozi wa Mfuko wa Arena kutoka Verona ambao umetoa mchango mkubwa katika kukuza na kudumisha Mapokeo na Tasaufi inayobubujika kutoka katika Kanisa, ili kuendeleza utamaduni, fasihi, muziki na sanaa katika maeneo haya. Utajiri huu ni amana kubwa inayopaswa kulindwa na kuhifadhiwa, ili kuwarithisha vijana wa kizazi kipya kwa siku za usoni.

Mti wa Noeli ni kielelezo cha Fumbo la Umwilisho na Mwanga wa Mataifa unaokuja kumwokoa mwanadamu na kufukuza giza katika maisha yake. Ni mti unaogusa udugu, upendo na mshikamano; urafiki na kwamba, hii ni changamoto kwa watu wa nyakati hizi kujikita katika kiasi na mshikamano wa upendo. Ni mwaliko wa kujenga na kudumisha umoja, maridhiano na amani; kuhakikisha watu wanatengeneza nafasi kwa Mwenyezi Mungu ili aweze kupata makazi katika maisha yao ya kila siku, ili hatimaye, waonje upendo wake. Mti wa Noeli ni kielelezo cha mwanga, matumaini na upendo.

Baba Mtakatifu amewatakia wajumbe wote kutoka Veneto na Calabria amani na utulivu katika maadhimisho ya Siku kuu ya Noeli, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, awaletee mwanga ili kupambana kikamilifu na dhambi, ili kumkirimia mwanadamu mwanga wa Kimungu ulioletwa na Yesu mwenyewe na kuwapatia matumaini wale wote wanaoteseka kutokana na kuelemewa na giza totoro katika undani wa maisha yao!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.