Askofu mkuu Ignatius Chama, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia anasema kwamba,
katika kipindi cha miaka 50 tangu Zambia ilipojipatia uhuru wake kutoka kwa Mwingereza,
kumekuwepo na mafanikio makubwa katika nyanja mbali mbali za maisha, ingawa utandawazi
bado unaendelea kuwatumbukiza Wazambia wengi katika dimbwi la umaskini wa hali na
kipato.
Zambia imebahatika
kuwa na rasilimali nyingi, lakini bado hazijatumika kikamilifu kwa ustawi na maendeleo
ya wananchi wote wa Zambia. Ugonjwa wa Ukimwi ni kikwazo kikubwa kwa maendeleo ya
familia nyingi, kwani athari zake ni kubwa kwa familia na jamii katika ujumla wake.
Askofu
mkuu Chama anasema, wananchi wa Zambia kwa sasa wako kwenye mchakato wa kampeni kwa
ajili ya kumpata Rais atakayemrithi, Marehemu Michael Chilufya Sata alifariki dunia
hivi karibuni, akiwa anapata matibabu nchini Uingereza. Lakini ikumbukwe kwamba, kunako
mwaka 2008 Zambia ilimpoteza pia Rais Levy Mwanawasa, wakati alipokuwa anahudhuria
mkutanio wa Umoja wa Afrika.
Katika kipindi cha siku tisini, kadiri ya Katiba,
wananchi wanapaswa kufanya uchaguzi, ndiyo maana kwa sasa Zambia ni patashika nguo
kuchanika, kila Rais mtarajiwa anaendelea kujinadi kwa Chama chake ili aweze kupewa
nafasi ya kupeperusha bendera wakati wa uchaguzi mkuu.
Zambia katika uwanja
wa kisiasa inaendelea kupita katika kipindi kigumu sana ingawa hawajafikia hatua ya
baadhi ya watu kuingia mstituni ili kuendesha mapambano ya silaha. Wananchi wamefikia
kiwango kikubwa cha ukomavu katika masuala ya kisiasa, lakini bado wanahitaji kuendelea
kukua na kukomaa zaidi, ili kutafuta mafao ya wengi, utu na heshima ya binadamu. Ili
kufikia ukomavu wa kisiasa kuna haja ya watu kuendelea kujifunza na kupima mafanikio
yao kwa hekima na busara zaidi.
Kanisa nchini Zambia kwa asili ni la Kimissionari,
lakini nalo pia linaendelea kukomaa kwani sehemu kubwa ya mihimili ya Uinjilishaji
ni Wazambia wenywe, jambo linaloonesha ukomavu katika kujitegemea na kulitegemeza
Kanisa katika rasilimali watu. Kanisa Katoliki nchini Zambia linaendelea kushiriki
kikamilifu katika mchakato wa Uinjilishaji wa watu kwa njia ya watawa mbali mbali
wanaofanya kazi ndani na nje ya Zambia na Afrika katika ujumla wake. Umissionari ni
sehemu ya vinasaba vya Kanisa Katoliki nchini Zambia.
Takwimu zinaonesha kwamba,
Kanisa Katoliki Zambia limewekeza sana katika sekta ya elimu, utume ulioanza kunako
mwaka 1895 kwa kuanzisha shule za awali, sekondari na vyuo vya ufundi. Lengo ni kuhakikisha
kwamba, Kanisa linashiriki kikamilifu katika majiundo ya mtu mzima: kiroho na kimwili,
kwa kumpatia elimu bora, itakayomwezesha kupambana na mazingira, ili Zambia iweze
kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.
Kanisa limewekeza sana katika sekta
ya afya, kiasi cha kujenga mtandao wa zahanati, vituo vya afya na hospitali, huduma
inayoratibiwa na Idara ya Afya ya Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia, kwa kushirikiana
na wadau mbali mbali katika sekta ya afya. Zambia ina hospitali 18 na Zahanati 38
na kwamba, asilimi 60% ya vituo vyote vya afya nchini humo, vinamilikiwa na kuendeshwa
na Kanisa Katoliki na vingi viko katika maeneo ya vijijini, huko ambako wengi hawataki
kwenda kutokana na ukata wa wananchi. Kanisa limeendelea kutoa huduma makini kwa wagonjwa
na waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi.
Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia, limeendelea
kuwekeza zaidi na zaidi katika maendeleo ya teknolojia ya habari, sekta inayoratibiwa
na Idara ya habari na mawasiliano ya Baraza la Maaskofu Katoliki Zambia. Kanisa linamiliki
na kuendesha vituo 7 vya Radio, vituo 5 ni vya majimbo na 2 ni vya Mashirika ya kitawa.
Baadhi ya majimbo yameanzisha mchakato wa kutaka kufungua vituo vya Radio, ili kuliwezesha
Kanisa kuwa ni sauti ya kinabii kwa kuwatetea wanyonge.
Na Padre Richard A.
Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.