2014-12-18 14:38:47

Onjeni upendo wa Kristo, ili kuwashirikisha wengine!


Baba Mtakatifu Francisko alipokutana na kuzungumza na Watoto wa Umoja wa Vijana Wakatoliki kutoka Italia waliofika mjini Vatican Alhamisi, tarehe 18 Desemba 2014 amewashukuru na kuwapongeza pamoja na kuwataka kusonga mbele kwa imani, matumaini na ujasiri mkubwa katika kugundua mpango wa Yesu katika maisha ya kila mtoto. Dhamana hii wanaitekeleza kwa kushirikiana na wazazi, marafiki, wenzi wa Katekesi na Michezo.

Baba Mtakatifu anawataka watoto hawa kuonesha kwamba, wanawajali watoto wenzao ambao wanaogelea katika umaskini na mazingira magumu ya maisha, kama kielelezo cha mapendo kwa jirani, ili kweli hija ya maisha yao iweze kujikita katika upendo. Watoto wanapaswa kulipenda Kanisa na viongozi wake pamoja na kujiweka tayari kuhudumia, kwa kushirikisha muda, nguvu, vipaji katika maisha na utume wa Parokia, ili kuonesha ushuhuda wa utajiri ambao Mwenyezi Mungu amewakirimia, ili kuwashirikisha na kuwaonjesha wengine.

Baba Mtakatifu anawataka watoto kuwa ni mitume wa amani na utulivu kwa kuwamegea jirani zao upendo, wakiwa wameungana na Yesu, kwa kufanya hivi, kila jambo linawezekana. Watoto wajenge na kuimarisha utamaduni wa kuzungumza na Yesu kwani yeye ni chemchemi ya furaha; msamaha na huruma wanapokosa, ili waweze kusimulia matendo makuu ya Mungu katika maisha yao. Noeli iwasaidie watoto hawa kuwa kweli ni mitume wa Yesu, kwa kumkubali katika maisha yao, kama alivyofanya Bikira Maria, alipokubali kuwa ni Mama wa Mungu.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.