2014-12-17 09:01:32

Mwachieni nafasi Yesu ili azaliwe tena ndani mwenu!


Kardinali Angelo Comastri, mhudumu mkuu wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumanne, tarehe 16 Desemba 2014 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya wafanyakazi wa Vatican, kama sehemu ya maandalizi ya Siku kuu ya Noeli, inayowakumbusha binadamu kwamba, Neno wa Mungu amefanyika mwili na kuzaliwa kati yao katika hali ya umaskini na unyenyekevu mkuu!

Yesu alizaliwa Pangoni, mahali pa kulishia wanyama! Swali la msingi ambalo Kardinali Comastri anauliza, Je, kwanini Yesu aliamua kuzaliwa katika mazingira duni kiasi hiki? Kimsingi, dunia ni sawa na tambara bovu, mahali panapoonesha umaskini mkubwa, ikiwa kama waamini na walimwengu hawatakuwa tayari kupokea mwanga kutoka kwa Kristo, ili kushuhudia matendo makuu ya Mungu yanayojikita katika toba na wongofu wa ndani; katika misingi ya haki, amani na mshikamano.

Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuondokana na ubinafsi unaopofusha mawazo na matendo ya watu, kiasi cha kushindwa kuona utu na heshima ya binadamu; mateso na mahangaiko ya watu mbali mbali. Noeli ni fursa makini kwa waamini kumwachia nafasi ili Mtoto Yesu aweze kuzaliwa ndani mwao, tayari kumshuhudia kwa njia ya imani tendaji!







All the contents on this site are copyrighted ©.