2014-12-17 09:25:58

Maaskofu Australia wasali kwa ajili ya watu waliofariki dunia huko Sydney!


Baraza la Maaskofu Katoliki Australia, Jumanne tarehe 16 Desemba 2014 limeadhimisha Ibada ya Sala maalum kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea watu waliofariki dunia kutokana na vitendo vya kigaidi vilivyofanywa mjini Sydney, Australia, siku ya jumatatu. Kitendo hiki kimefanywa na Man Haron Monis, mwamini mwenye msimamo mkali wa kidini kutoka Iran aliyeteka watu kadhaa nyara kwa kipindi cha masaa kumi na sita.

Katika shambulio hili la kigaidi, watu watatu wamepoteza maisha yao! Baraza la Maaskofu Katoliki Australia linaungana na wale wote wanaoomboleza msiba huu mkubwa kwa kuondokewa na ndugu zao. Maaskofu wanavishukuru na kuvipongeza vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutekeleza wajibu wao kwa kuhatarisha maisha yao, ili kuokoa maisha ya wananchi wengi wa Australia kutoka katika tukio hili la kigaidi. Maaskofu wanawapongeza wafanyakazi katika sekta ya afya waliotekeleza dhamana yao kwa utashi kamili, uvumilivu na ujasiri.

Baraza la Maaskofu Katoliki Australia linawaalika wananchi na watu wote wenye mapenzi mema kulaani vikali vitendo vya kigaidi, hasa wakati huu Wakristo wanapojiandaa kwa ajili ya kuadhimisha Siku kuu ya Noeli; iwe ni fursa ya kutafuta, kujenga na kudumisha amani na maelewano kati ya watu. Ni fursa ya kuwaendea wote kwa kutumia nguvu ya upendo, ili kuwaonjesha amani na uponyaji!







All the contents on this site are copyrighted ©.