2014-12-15 09:30:32

Jengeni na kudumisha umoja wa Wakristo!


Mpendwa msikilizaji wa kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, Tumsifu Yesu Kristo! Tupo katika mwendelezo wetu wa kudadafua hati za mtanguso Mkuu wa pili wa Vaticani, ili kuweza kuuleta ujumbe wake katika Kanisa la Nyumbani. RealAudioMP3

Leo tunalitazama agizo la mababa wa Mtaguso liitwalo kwa lugha ya kilatini Unitatis Redintegratio, inayohusu urudishaji wa umoja kati ya Wakristo. Mababa waliitazama historia ya Kanisa la Kristo na kuona jinsi ambavyo kumekuwa na mimegeko katika vipindi mbalimbali vya historia. Mimegeko na migawanyiko hiyo mababa wanaitazama kama makwazo makubwa kwa ulimwengu na hivyo kufanya ulimwengu usiweze kuamini Injili ya Kristo.

Tumegawanyika kana kwambwa Kristo aligawanyika! Tunasemanasemana, hatupendani wala kuheshimiana. Na katika kutengana kwetu, wakati mwingine tunashambuliana kwa neno hilohio la Kristo. Hayo ni makwazo kwa ulimwengu. Ni kama tumeukata mwili wa Kristo katika vipandevipande. Kristo Yesu aliyetumwa na Baba tangu milele, kwa njia ya roho wake alipenda tuwe kitu kimoja na ndiyo maana alisali akituombea umoja. Lakini katika ubinadamu wetu, tumekengeuka matakwa hayo ya Kristo Yesu.

Mababa wa Mtaguso, wakisukumwa na dhamiri wajibifu mbele za Mungu mmoja na wa Kweli, kwa njia ya hati hii wanatufundisha na kutuhimiza sisi sote kujitahidi kujenga ushirikiano na wenzetu wengineo wanaomwamini Kristo. Kurudisha umoja kati ya Wakristo wote kwa njia ya ushirikiano makini, ni moja ya malengo ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican.

Kwa njia ya Mtaguso huu, Mungu ametupatia mwanga wa Uekumeni. Badala ya kusema turudi tuwe kitu kimoja, tunasema tushirikiane katika umoja wa kweli huku tukiheshimu tofauti zetu. Yapo mambo ya msingi ambayo yanaweza kutuweka katika meza moja. Kwa agizo la hati hii, Kanisa Katoliki linapaswa kushirikiana na madhehebu yoyote ya Kikristo, ili kutoa mwanya zaidi kwa kazi ya Roho Mtakatifu. Ni katika mtazamo huu, Kanisa Katoliki, linaona ishara chanya za kazi ya Roho Mtakatifu na hata tunu za wokovu katika madhehebu mengine ya Kikristo.

Sura ya kwanza inaeleza msimamo wa Kanisa Katoliki kuhusu Uekumeni. Mababa wanatufundisha kwamba Kanisa ni moja tu, ambalo Kristo Bwana alilijenga juu ya mitume, nalo limekabidhiwa kwa waandamizi wa mitume chini ya Warithi wa Mtume Petro (yaani Mababa Watakatifu). Wakristo wa madhehebu mengine, ni Wakristo halisi, ijapo kuwa hawapo katika ushirika kamili na sisi.

Mababa wanatualika tuwaheshimu, tushirikiane nao. Nao pia katika imani yao, wanapiga mbio kumwelekea Mungu yuleyule mmoja na wa kweli. Makanisa yao au jumuia zao vinatumiwa na Mungu kama vyombo vya wokovu, ila katika Kanisa Katoliki tu unapatikana ukweli mzima na tunu zote za ukombozi. Hata hivyo tunakiri kwamba kwa nafasi fulani, hatutumii vizuri neema hizo hata tunawakwaza wenzetu. Kwa fundisho la hati hii, tulenge ukamilifu wa Kikristo ili Kanisa ling’ae mbele ya wote. Mbali ya matendo ya kupendana ni muhimu pia kuwa na majadiliano ya kitaali-Mungu na mikutaniko ya sala ya pamoja.

Sura ya pili inatuelekeza kuwa ni jukumu letu sisi sote kutekeleza umoja huo kwa njia ya kurekebisha mapungufu ndani ya Kanisa, kuuambata uongofu wa kweli, kusali, kushirikishana sakramenti, kufahamiana, kueleza imani kwa ufasaha na bila kudharau madhehebu mengine, kushirikiana katika kutetea haki na amani na kuleta maendeleo. Tushikamane kuukuza na kuulinda Ukristo wetu.

Mpendwa msikilizaji wa Kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, mimi na wewe ndio wadau wa kuleta umoja wa Kikristo. Mababa wa Mtaguso wametuelekeza kuwa ni jukumu letu sisi sote. Tunaleta ujumbe huu kwenye familia tukiamini kuwa watu wote, waungwana kwa wakorofi wanatoka katika familia. Watoto wetu wakifundishwa imani ya kweli, hawatakuwa na sababu ya kudharau Wakristo wa madhehebu mengine.

Ni aibu kubwa sana nyakati zetu hizi sisi Wakristo tunapoanza kupigana vijembe majukwaani, kwa kunadi madhehebu yetu kana kwamba ndiyo yana Kristo zaidi kuliko wengine. Hayo ni makwazo kwa ulimwengu. Tukiwafundisha dini vizuri watoto wetu daima watajua thamani na wajibu wa kuilinda imani ya baba zetu, imani ya kweli Katoliki, bila kukwaruzana na wengine.

Ni mwito kwetu sote katika familia na katika ujirani, tuheshimiane, tupendane, na kwa busara tushirikiane katika mambo ya imani zetu bila kuvuka mipaka yetu. Wale tunaowashambulia Wakristo wenzetu kwa kejeli na vijembe kana kwamba wamepotea kabisa, hiyo ni dalili wazi kuwa bado hatuijui dini yetu. Dini yetu sio ya watu wakorofi. Ni dini takatifu, ya upendo na amani. Na wewe Mkatoliki huna haja ya kuanza kushambuliana na mtu anayekutuhumu juu ya imani yako katika Ekaristi, Msalaba, Bikira Maria, Baba Mtakatifu nk. Hayo hayawahusu. Kila mtu ale ugali kimyakimya upande wake.

Mkatoliki, ionee fahari imani yako, tembea kifua mbele kwa sababu unamsadiki Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai. Ila, tunza kichwa! Sio lazima ujibu kila swali na kejeli unayoulizwa. Ila ujitahidi sana, uifahamu imani yako vizuri, ili akitokea mtu anakuuliza kwa kutaka kuelewa, mjibu na umfundishe kwa upole hadi aelewe. Ila mkejeli na mchokozi, mjibu kwa kukaa kimya tu, na kumheshimu basi.

Ukiona mtu anadodosoadodosoa imani yako kwa uchokozi huku amekufungia maspika-mzinga jukwaani, jua kuwa hana sera za dini yake. Hao tuwaombee tu kimyakimya, bila kugombana. Sasa ikitokea wewe Mkatoliki, imani yako huijui, ni mwigizaji, na anayekuchokoza naye hajui ya kwake, ni mfuata mkumbo tu, halafu mnaingia katika mjadala wa mambo msiyoyajua, hapo lazima kutakuwa na kelele nyingi tena kwa sauti kubwa zenye kuzaa matusi na mfarakano.

Kazi ya kulinda umoja uliodhamiriwa na Kristo katika Kanisa, ni jukumu letu sote. Lakini hatutaweza kwa nguvu zetu peke yetu. Hati hii inatuelekeza kuwa tunahitaji msaada wa Mungu mwenyewe. Roho wa umoja atuangaze na kutuongoza. Wakati mwinginge, kazi ya kuleta umoja na ushirikiano mwema inakwamishwa na midomo yetu na matumbo yetu. Wengi tunasahau lengo la Kristo, badala yake tunaweka mbele ubinafsi wetu. Hapo tunakwamisha Injili ya Kristo! Ni katika roho na sala na dhamiri njema tutaweza kufikia lengo wanalotuelekeza Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican

Kutoka katika Studio za Radio Vaticani, ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB








All the contents on this site are copyrighted ©.