2014-12-15 09:07:42

Atema cheche!


Askofu Renatus Nkwande wa Jimbo Katoliki Bunda katika maaadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu Jumapili iliyopita tarehe 14 Desemba 2014 kwenye Parokia ya Mwili na Damu ya Kristo, iliyoko Jimbo kuu la Roma, kwa ajili ya Jumuiya ya Wanafunzi Watanzania Wakatoliki wanaosoma na kuishi mjini Roma, amewataka watanzania kuendelea kuombea misingi ya: haki, amani na utulivu hasa wakati huu Tanzania inapokabiliwa na majaribu makubwa katika historia na maisha yake. RealAudioMP3

Askofu Nkwande, ametumia fursa ya Ibada ya Jumapili, kwa ajili ya kuombea uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliokuwa unafanyika nchini Tanzania kwa kuvishirikisha vyama mbali mbali vya kisiasa. Tanzania kwa kipindi cha miaka 53 iliyopita, ilihesabiwa kuwa ni nchi ya amani, lakini leo hii, wengi wanasema Tanzania ni nchi yenye utulivu.

Ameombea uchaguzi wa Serikali za mitaa, ili kweli Jamii ya Watanzania iweze kupata viongozi: wema na waadilifu; wakweli na waaminifu; watu wenye nia ya kuchochea maendeleo kwa watu, huku wakijenga na kudumisha umoja, upendo na mshikamano kati ya watu kuliko kuendekeza udini, ukabila na umajimbo; mambo ambayo yanaweza kulitumbukiza taifa la Tanzania katika majanga makubwa.

Askofu Nkwande anasema: misimamo mikali ya kidini, mauaji, dhuluma na vistisho kwa viongozi wa kidini; madai yasiyokuwa kweli kuhusu baadhi ya watanzania kukandamizwa kwa misingi ya udini; rushwa, wizi na ufisadi ni dalili kwamba, amani na utulivu nchini Tanzania vinaweza kutoweka kama ndoto ya mchana, ikiwa kama watanzania wenyewe hawatasimama kidete kupinga chokochoko hizi kwa kukazia: ukweli, umoja na mshikamano wa kitaifa.

Hapa Askofu Nkwande anawataka pia viongozi wa Kanisa kuchunguza dhamiri zao mbele ya Mwenyezi Mungu kuona ikiwa kama kweli, wamekuwa ni mfano bora wa kuigwa kwa njia ya maisha na matendo yao, ili kweli waweze kuwa na ujasiri wa kukemea maovu yanapojitokeza katika jamii, vinginevyo watakuwa ni mashuhuda wasiokuwa na mvuto wala mashiko, tofauti kabisa na alivyokuwa Yohane Mbatizaji anayesimuliwa katika Liturujia ya Neno la Mungu, Jumapili ya tatu ya Kipindi cha Majilio.

Askofu Nkwande amesema, Kashfa ya Fedha za Escrow imelitikisa Taifa hata Kanisa limeguswa, kwani kuna baadhi ya viongozi wa Kanisa wametajwa kupokea mafungu makubwa makubwa ya fedha kutoka kwenye akaunti ya Escrow ya Tegeta. Kashfa hii iwe ni fundisho kwa Kanisa kwamba, kamwe halitaweza kujitolesheleza, litaendelea kutaabika na kuchakarika, huku likiwezeshwa na waamini wa kawaida kabisa kama ilivyotokea kwa Yesu na Mitume wake.

Vinginevyo, anasema Askofu Nkwande, harambee zinazoitishwa na Makanisa zinaweza kukusanya maelfu ya fedha chafu, kiasi kwamba, Makanisa, majumba na mambo mengine ya Kanisa yatakuwa yananuka harufu ya fedha chafu. Umaskini na ukata wa Kanisa, kisiwe ni kisingizio cha kukengeuka na kuacha misingi ya maadili, uwajibikaji, ukweli na uwazi.

Jumapili iliyopita Jumuiya ya Wanafunzi Wakatoliki kutoka Tanzania wanaosoma mjini Roma ilifanya uchaguzi mkuu na wafuatao wamepewa ridhaa ya kuwaongoza watanzania wenzao kwa kipindi cha mwaka mmoja yaani 2014- 2014.

1. Pd. Joseph Peter Mosha, M-Kiti
2. Pd. Pambo Martin Mkorwe OSB, Katibu.
3. Sr. Martin Shayo CDNK, Fedha.
4. Pd. Sayoni Jeremiah SDS, Liturujia na Ibada.
5. Pd. Klement Kihiyo, Mkutubi.

Imeandikwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.