2014-12-13 14:30:36

Vatican na Serikali ya Italia kuendelea kushirikiana kwa karibu zaidi!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, tarehe 13 Desemba 2014 amekutana na kuzungumza na Bwana Matteo Renzi, Waziri mkuu wa Italia pamoja na ujumbe wake, ambao baadaye walikutana kuzungumza na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti aliyekuwa Katibu mkuu wa Mambo ya nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa mjini Vatican.

Viongozi hawa wawili wamejadili kwa kina na mapana kuhusu athari za myumbo wa uchumi kimataifa zinavyotendea mahusiano ya kijamii, kiasi cha kuzalisha kundi kubwa la vijana ambao hawana fursa za ajira. Baba Mtakatifu na mgeni wake, wamekazia umuhimu wa elimu na majiundo makini kwa vijana wa kizazi kipya. Baadaye, viongozi hawa wamejikita katika masuala ya siasa kimataifa hasa kutokana na kuendelea kuwepo kwa kinzani na vita sehemu mbali mbali za dunia.

Italia imepongeza hotuba iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati alipotembelea Bunge la Ulaya huko Strasbourg, Ufaransa hivi karibuni na kwamba, mambo yaliyotajwa na Baba Mtakatifu ni kichocheo kikubwa cha maendeleo na mshikamano na mfungamano kati ya watu. Vatican na Italia zimerudia tena wito wa kuendelea kushirikiana kwa karibu zaidi, ili kutafuta ufumbuzi wa matatizo na changamoto zinazojitokeza baina ya pande hizi mbili!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican







All the contents on this site are copyrighted ©.