2014-12-13 09:10:25

Maandalizi ya Siku ya Familia Kimataifa yaanza kushika kasi!


Baraza la Maaskofu Katoliki Slovacchia, linaendelea kukitumia Kipindi cha Majilio ambacho kinasheheni, imani, matumaini na mapendo, kama sehemu ya maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Familia Duniani, itakayofanyika Jimbo kuu la Philadelfia, Marekani, Mwezi Septemba 2015 kwa ushiriki wa Baba Mtakatifu Francisko.

Baraza la Maaskofu Katoliki Slovacchia kwa kushirikiana na Jimbo kuu la Philadelphia, limekuwa likiendesha Katekesi kuhusu maisha ya ndoa na familia; majiundo makini yanayojichimbia katika kauli mbiu "Upendo ni utume wetu; familia ni utimilifu wa maisha". Katekesi hizi ambazo zinasambazwa pia kwa kutumia mitandao ya kijamii, zinalenga kuisaidia Familia ya Mungu nchini Slovacchia, kutambua, kuthamini na kudumisha misingi bora ya maisha ya ndoa na familia, tayari kutoka kifua mbele ili kuwatangazia Watu wa Mataifa, Injili ya Familia.

Maadhimisho ya Siku ya Familia Kimataifa, ni tukio ambalo linakwenda sanjari na maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu familia, ambayo awamu yake ya kwanza tayari imekwisha adhimishwa na sasa waamini wanaendelea kutafakari, ili kuwasaidia Mababa wa Sinodi kuibua mbinu mkakati utakaoziwezesha Familia za Kikristo kutekeleza wito na utume wao ndani ya Kanisa na katika ulimwengu mamboleo!

Katekesi hizi za kina zinapata chimbuko lake kutoka katika: Maandiko Matakatifu, Mafundisho na Mapokeo ya Kanisa, ili kuonesha utajiri mkubwa wa imani katika Kristo na Kanisa lake kuhusiana na maisha ya Sakramenti ya Ndoa na Familia. Maaskofu Katoliki Slovacchia wanawaalika Wakristo kuanzisha na kuendeleza majadiliano yanayohusu: umuhimu wa maisha ya Sakramenti ya Ndoa na Familia pamoja na changamoto zake, ili kweli waweze kuchangia katika kuenzi tunu msingi za maisha ya Ndoa na Familia, ambazo kwa sasa zinakabiliwa na changamoto kubwa kutokana na watu kumezwa mno na malimwengu, kwa kukumbatia utamaduni wa kifo, mmomonyoko wa tunu msingi za maisha ya kiutu na kimaadili, kwa kisingizio cha uhuru binafsi.

Ushiriki wa waamini na wadau kutoka sehemu mbali mbali katika Maadhimisho ya Siku ya Familia huko Philadelfia, inaweza kuwa ni fursa kwa waamini kushirikishana uzoefu, mang'amuzi, changamoto na matumaini katika mchakato wa kukuza na kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.