2014-12-12 08:22:12

Umaskini ni kikwazo cha maendeleo nchini Zimbabwe!


Viongozi wengi wa Zimbabwe wanagombania madaraka na kusahau kwamba, kuna maelfu ya wananchi wa Zimbabwe wanaoogelea katika dimbwi la umaskini wa hali na kipato na kwamba, umaskini ni kikwazo kikubwa cha maendeleo ya wananchi wengi wa Zimbabwe. Kuna maelfu ya wananchi wa Zimbabwe wamekimbilia katika nchi jirani kama vile: Botswana, Msumbiji, Zambia na Afrika ya Kusini ili kutafuta riziki ya maisha.

Kwa wananchi waliobahatika kutoka nje ya Zimbabwe wanaendelea kuzisaidia familia zao kwa kuwatumia fedha, lakini si kila familia imebahatika kuwa na fursa hii! Lakini viongozi wa Kidini wanapozungumzia hali ya umaskini na ukosefu wa haki msingi za binadamu nchini Zimbabwe wanatishiwa maisha na wakati mwingine wanakiona cha mtema kuni! Viwanda vingi vimefungwa; mashamba yaliyotaifishwa na Serikali yamegeuka kuwa ni misitu ya wanyama pori.

Padre Felix Tachiona Mukaro kutoka Zimbabwe katika mahojiano maalum na Shirika la Kipapa la Misaada kwa Makanisa hitaji anasema kwamba, wananchi wengi wa Zimbabwe hawatarajii kupata mabadiliko makubwa ya kisiasa katika kipindi kifupi, lakini jambo la msingi ambalo linapaswa kupewa msukumo wa pekee ni mabadiliko ya kifikra; kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa ustawi, maendeleo na mafao ya wengi; mambo yanayojikita katika utu na heshima ya binadamu pamoja na kuheshimu haki zake msingi.

Kanisa nchini Zimbabwe linaendelea kuchangia katika ustawi na maendeleo ya wananchi kwa kutumia rasilimali yake "kiduchu" iliyopo kwa wakati huu. Lakini hata Kanisa pia linakabiliwa na hali ngumu ya uchumi, lakini bado liko imara katika kuwatangazia watu waliopendeka na kuvunjika moyo, Injili ya Matumaini.







All the contents on this site are copyrighted ©.