Uchaguzi mkuu kisiwe ni kikwazo cha maendeleo ya demokrasia nchini Burundi
Baraza la Maaskofu Katoliki Burundi katika ujumbe wake kwa waamini na watu wote nchini
humo katika kipindi hiki wanapojiandaa kwa ajili ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika
nchini Burundi kunako mwaka 2015, wanapenda kuchukua fursa hii kuwapongeza wananchi
ambao kwa njia ya kupiga kura wanafanya mabadiliko katika Serikali kwa kuwachagua
viongozi wanaowataka.
Hii ni sehemu ya utekelezaji wa haki yao msingi Kikatiba
pamoja na kudumisha msingi wa demokrasia na maendeleo ya kweli! Kanisa linathamini
mfumo wa demokrasia kwa sababu unawahakikishia wananchi ushiriki wao katika maamuzi
ya kisiasa, uwezekano wa kuchagua na kuwawajibisha viongozi wao sanjari na kuwabadilisha
kwa njia ya amani wakati unapowadia.
Demokrasia ya kweli inawezekana tu pale
Serikali inapotawala kwa kuzingatia sheria, utu na heshima ya binadamu. Uchaguzi ni
wajibu na haki ya kila mwananchi kwa mujibu wa sheria sanjari na kupima mafanikio,
matatizo na changamoto zilizojitokeza katika uongozi uliopita.
Baraza la Maaskofu
Katoliki Burundi linawapongeza wananchi kwa ukomavu wa kisiasa unaojionesha kwa njia
ya ushiriki wa kupiga kura kwani hadi sasa hakuna mtu ambaye amesusia kushiriki katika
uchaguzi mkuu kadiri ulivyopangwa na vyama vya kisiasa. Maaskofu wanasema, kwa sasa
kuna hali ambazo zinatishia majadiliano ya kisiasa, mbinu na mikakati ya uchaguzi
kuelemea upande mmoja tu, jambo ambalo linaweza kuwa ni hatari kubwa kwa mustakabali,
umoja na mshikamano wa kitaifa.
Wananchi wa Burundi wanajiandaa kushiriki katika
mchakato wa upigaji kura, huku amani na usalama wa wananchi viko mashakani. Kuna makundi
ya watu yanayoteka watu nyara na kuwapora; yanayoua bila huruma pamoja na kuendelea
kufanya uhalifu pamoja na kutumia lugha ambayo inachochea uvunjifu wa amani na usalama.
Inaonekana kana kwamba, kuna vijana ambao wako tayari kutumiwa na baadhi ya wanasiasa
kufanya vurugu nchini Burundi.
Baraza la Maaskofu Katoliki Burundi, linawataka
wananchi wote wa Burundi katika ujumla wao kuhakikisha kwamba, wanawajibika barabara
katika maamuzi na matendo yao, ili kweli uchaguzi mkuu nchini humo uweze kuwa huru,
kweli na wazi; uchaguzi unaozingatia sheria na demokrasia ya kweli. Uchaguzi mkuu
usiwe ni kikwazo cha maendeleo ya demokrasia nchini Burundi, bali chachu ya kujenga
na kuimarisha demokrasia na utawala wa sheria!
Na Padre Richard A. Mjigwa,
C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.