Rais Jakaya Kikwete kutoa maamuzi ya Escrow katika wiki moja Apokea Ripoti, nyaraka
na maazimio ya Bunge Aagiza Ripoti ya CAG iwekwe wazi hadharani, haya ni kati ya masuala
tete tunayokutaka uyasome kwa umakini!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amepokea Ripoti, nyaraka na ushauri wa Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania kuhusu Akaunti ya Tegeta Escrow na atavifanyia maamuzi katika
wiki moja ijayo. Rais Kikwete ambaye alianza kazi Jumatatu, Desemba 8, 2014 baada
ya mapumziko ya kufuatia upasuaji aliofanyiwa mwezi uliopita, amepokea Ripoti ya Mdhibiti
na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ripoti ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za
Umma (PAC) na Maazimio ya Bunge kuhusu Akaunti ya Tegeta Escrow.
Kufuatia kupokea
nyaraka hizo, Rais Kikwete ameelekeza kuwa Ripoti ya CAG iwekwe hadharani kwa ajili
ya umma kuweza kuisoma na kujua nini hasa kimesemwa na kupendekezwa na Mdhibiti na
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Rais Kikwete ameelekeza kuwa Ripoti hiyo itangazwe
kwenye magazeti yanayosomwa na watu wengi na kwenye mitandao ya kijamii, ili Ripoti
hiyo iweze kupatikana kwa Watanzania wengi.
Rais Kikwete ameanza kupitia na
kusoma nyaraka hizo na katika wiki moja ijayo atazitolea maamuzi kwa maana ya kwamba
yale mambo yanayomhusu yeye moja kwa moja atayatolea maamuzi yeye, yale yanayohusu
Serikali atayatolea maagizo na maelekezo ya namna ya kuyashughulikia.
Wakati
huo huo, Rais Kikwete Jumatatu, Desemba 8, 2014, alianza kazi rasmi baada ya afya
yake kuimarika kufuatia upasuaji aliofanyiwa mwezi uliopita. Mhe. Rais alianza kazi
rasmi kwa kumwapisha Mkuu mpya wa Mkoa wa Arusha, Mheshimiwa Daudi Felix Ntibenda
katika shughuli fupi iliyofanyika Ikulu, Dar Es Salaam. Kwa kuanzia Mhe. Rais atakuwa
anafanya kazi za ofisini na kwa muda mchache. Muda na kasi ya kufanya kazi ya Mhe.
Rais vitaongezeka kwa kadri afya yake inavyozidi kuimarika.
Na kwa sababu sasa
ameanza kazi, Mhe. Rais ataanza kushughulikia mambo yale ambayo yamekuwa yanasubiri
maamuzi yake. Rais Kikwete alifanyiwa upasuaji wa tezi dume katika Hospitali ya Johns
Hopkins ya Baltimore, Maryland, Marekani Novemba 8, mwaka huu na alirejea nyumbani
Novemba 29, mwaka huu. Tokea awasili nyumbani, Mhe. Rais amekuwa anafanya mazoezi
asubuhi na jioni kuimarisha afya yake kama alivyoshauriwa na madaktari.
Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete usiku wa Jumatatu,
Desemba 8, 2014 amepokea ujumbe wa viongozi wa dini wa Mkoa wa Dar Es salaam, ukiongozwa
kwa pamoja na Askofu Valentino Mokiwa wa Kanisa la Anglikana na Sheikh wa Mkoa wa
DSM, Alhaj Alhad Mussa Salum. Viongozi hao walifika Ikulu, Dar Es Salaam kumjulia
hali Rais Kikwete kufuatia upasuaji ambao alifanyiwa mwezi uliopita kwenye Hospitali
ya Johns Hopkins, Baltimore, Maryland, Marekani. Mbali na kumjulia hali, viongozi
hao pia walimwombea dua na sala wakiomba Mwenyezi Mungu amjalie kasi ya kurejesha
afya yake kamili na kuweza kuendelea na kazi ya kuwahudumia Watanzania. Rais Kikwete
pia alitumia muda huo kuwaelezea viongozi hao kuhusu ugonjwa uliokuwa unamsibu na
kusisitiza kuwa anakusudia kuchukua hatua zaidi za kuwahamasisha Watanzania kupima
afya zao mapema ili kujua fika hali za afya zao.
“Mimi Mwenyezi Mungu aliniongoza
kuweza kupima mapema na kugundua kuwa ilibidi nipatiwe matibabu ya haraka kuhusu saratani
ya tezi dume (prostrate). Vinginevyo nisingejua. Nawashukuru kwa maombi yenu, nawashukuru
kwa dua zenu. Daktari mkubwa ni Mungu na ndiye aliniongoza kufanya vipimo mapema,”
amesema Rais Kikwete na kuongeza:
“Kwa hakika, saratani inatibika lakini ni
lazima igundulike mapema na inaweza kugundulika mapema kama tukifanya uchunguzi wa
mara kwa mara wa afya zetu. Mimi nimenusurika kwa sababu nilipima mapema. Nataka tuanze
kuwasaidia watu wengi zaidi wapime afya zao mapema.”