Ujambazi unatishia amani na usalama wa wananchi Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati!
Baraza la Maaskofu Katoliki Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati, CAR, katika ujumbe
wake kwa waamini katika kipindi hiki cha Majilio wanasema kwamba, vitendo vya uhalifu,
ujambazi na unyang’anyi wa kutumia silaha ni mambo ambayo yanakwamisha mchakato wa
ujenzi wa misingi ya haki, amani na utulivu nchini humo. Kuna watu ambao wanatekwa
nyara na watu wenye silaha hali ambayo inajenga hofu na wasi wasi kwa wananchi kuweza
kutekeleza shughuli zao za kila siku kwa kuhofia usalama wa maisha na mali zao.
Kuna
baadhi ya watu wamelazimika kuyakimbia makazi yao, ili kutafuta usalama sehemu nyingine
za nchi, hasa Bangui, Bambari na Batangafo. Kinzani zilizojitokeza kati ya waasi wa
Seleka na Balaka zimepelekea mgawanyiko na mpasuko wa kitaifa, hali ambayo imetishia
umoja na mfungamano wa kitaifa, kwa misingi ya udini. Hapa ikaonekana kwamba, kuna
vita kati ya waamini wa dini ya Kiislam na dini ya Kikristo, jambo ambalo halikuwa
na ukweli wowote ule.
Lakini ikumbukwe kwamba, Waislam na Wakristo kwa miaka
mingi wameishi kwa amani na utulivu; kwa upendo na mshikamano, huku watu wakisaidiana
kwa hali na mali. Vurugu zenye mwelekeo wa kidini ni matokeo ya baadhi ya waamini
kuwa na misimamo mikali ya kiimani, hali inayohatarisha uhuru wa kuabudu na matokeo
yake ni kuvunjika kwa haki msingi za binadamu, kunakopelekea mauaji ya watu wasiokuwa
na hatia.
Makubaliano yaliyofikiwa kati ya Kikundi cha Seleka na Balaka, ili
kusitisha vita, kinzani na mauaji ya watu wasiokuwa na hatia hayana budi kutekelezwa
pamoja na kuhakikisha kwamba, Serikali inawashughulikia kikamilifu watu wanaojihusisha
na magenge ya kihalifu, ili utawala wa sheria uweze kuchukua mkondo wake, ili watu
waishi kwa amani na utulivu.
Maaskofu wanakumbusha kwamba, amani ni zawadi
kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayomwajibisha mwanadamu. Amani inaweza kulindwa
na kudumishwa kwa misingi ya majadiliano yanayojikita katika ukweli na uwazi, mafao
ya wengi na haki msingi za binadamu.