Baba Mtakatifu Francisko , Jumapili jioni, alipeleka salaam na ujumbe wake wa matashi
mema, kwa wakazi wa mji wa Gubbio , Kaskazini mwa Italia, ambako kila mwaka, sasa
kumekuwa na utamaduni maalum wa kuwasha taa za mti Noel, Mti ulio mkubwa, kuliko
miti yote ya Noel Dunia. Mti wa Noel ishara maalum ya kipindi cha Noel, kipindi
cha kuzaliwa kwa mkombozi wa dunia.
Katika ujumbe huo, Papa amesema, wakati
wa kuwasha taa za pango la Noel, tunacholenga zaidi ni kusema kwamba mwanga wa Kristo
umo ndani yetu. Papa amesisitiza , Noel bila mwanga si Noel. Kwa jinsi tunavyowasha
taa katika mti wa Noel , naiwe hivyo pia kuwasha mwanga katika roho zetu , katika
mioyo yetu , ili kuonyesha ishara ya kusamehe wengine; na kwamba hakuna uadui unaotia
tena giza la chuki na fitina moyoni. Kwamba kuna mwanga wa Yesu ndani ya moyo, ambao
ni upendo na kusamehe. Papa ameomba ili kwamba hamu hii iwe kwa wote, kwamba, hiki
ni kipindi cha kuwasha upya mwanga wa Kristo, mahali penye Pango.
Papa Francisko
, amewashukuru wote kwa zawadi yao ya kujitolea kufanikisha tukio hili, ishara ya
upendo wa Kristo aliyejitolea pia kwa ajili ya wokovu wetu. Kwao wote amewatakia
heri, amani na furaha za dhati , ili kwamba, giza lisitawale tena nafsi , bali iwe
sala na maombi kwa Bwana wa Msamaha. Huu ni wakati wa Noel, nafasi kubwa ya kufanya
safi roho, na hakuna sababu ya kuwa na hofu, kumwendea Kuhani, mwenye huruma, mwenye
kusamehe yote katika jina la Mungu, kwa sababu Mungu husamehe kila kitu.
Papa
ametolea ombi lake ili kwamba, Mwanga huu uwe katika nyoyo za wote, katika familia
zote, na katika mji huo wa Gubbio. Kwa imani huo Papa kwa kutumia teknolojia ya
Tablet, tokea Makazi ya jengo la Mtakatifu Marta, la ndani ya Vatican, aliwasha taa
za Mti wa Noel wa Gubbio, na kutoa Baraka za Kipapa kwa kumwomba Mwenyezi Mungu,
Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, akisema Heri za Noel kwenu nyote, na pia mkumbuke
kuomba kwa ajili yangu. Sherehe ya mwaka huu ya kuwasha taa za mti huu wa Noel
wa Gubbio, ziliandaliwa katika uwanja wa Wafia dini wa Gubbio na kuuunganishwa katika
mtandao wa video wa Kituo cha Televisheni cha Vatican , ili kuliwezesha watu kufuatilia
sherehe hizi , kumwona Papa akiwasha taa za mti wa Noel wa Gubbio tokea Vatican.
Sherehe ya Mti Noel wa Gubbio, zilianzishwa tangu mwaka 1981, tangu hapo
hufanyika kila mwaka katika mji huo , kwa kufanikishwa na kundi la kujitolea la watu
wanaoishi katika mteremko wa mlima Ingino, unaoelekea mji wa Gubbio, Mkoani Umbria.
Tangu mwaka 1991, uliingia kitabu cha kumbukumbu cha utendaji usiokuwa wa kawaida
Guinness Records. Papa Benedict XVI pia aliwasha taa za mti wa Gubbio mwaka 2011
na Rais wa Jamhuri ya Italia Giorgio Napolitano, aliwasha taa katika mti huo mwaka
2012. Taa za mti huu huendelea kuwashwa hadi jioni ya Januari 6.