2014-12-08 10:57:46

Kanisa liko mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya Ukimwi


Baraza la Maaskofu Katoliki Uganda, tangu mwaka 1989 limekuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi nchini Uganda, kwa kuhakikisha kwamba, Watu wa Mungu wanapatiwa huduma makini, kwa kujali na kuzingatia heshima na utu wao kama binadamu. Kwa kufanya hivi Kanisa linatambua sura ya Kristo mteswa kati ya wagonjwa, lakini zaidi wagonjwa wa Ukimwi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Uganda limekuwa likijitahidi kukusanya takwimu za wagonjwa wa Ukimwi na wale wanaohudumiwa katika vituo vinavyosimamiwa na kuendeshwa na Kanisa. Hadi sasa kuna zaidi ya wagonjwa 90, 646 wanaohudumiwa katika vituo hivi, ingawa bado kuna vituo ambavyo havijaanza kutoa takwimu zake katika idara ya takwimu za Kanisa Katoliki Uganda, unaojulikana kama DHIS2.

Makanisa mahalia nchini Uganda kwa kutumia vituo vyake vya afya, yanaendelea kutoa huduma kwa Mama na mwana, ili kudhibiti maambukizi ya virusi kutoka kwa Mama mjamzito kwenda kwa mtoto wakati wa kujifungua na kampeni hii imesaidia kuokoa maisha ya watoto wengi ambao kwa sasa wanazaliwa pasi na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi. Lengo ni kuhakikisha kwamba, walau Uganda inafanikiwa kuzuia maambukizi ya Virusi vya Ukimwi kutoka kwa Mama kwenda kwa mtoto. Ili kuweza kufikia lengo hili kila mdau anapaswa kutekeleza kikamilifu dhamana na wajibu wake mbele ya umma na familia katika ujumla wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.