Huruma, upendo na mshikamano ndiyo ujumbe wa Noeli kwa Mwaka 2014
Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican, Jumamosi, tarehe 6 Desemba 2014
ametembelea Hospitali ya Bambino Gesù inamilikiwa na kuendeshwa na Vatican, ili kuwasalimia
watoto waliolazwa Hospitalini hapo pamoja na kuwatakia kheri na baraka kwa ajili ya
Siku kuu ya Noeli na Mwaka mpya wa 2015. Kardinali Parolin alipowasili Hospitalini
hapo amepokelewa na viongozi wakuu wa Hospitali ya Bambino Gesù pamoja na kuzungumza
na wazazi na watoto wagonjwa waliolazwa Hospitalini hapo.
Kardinali Parolin
akiwa ameambatana na viongozi wa Hospitali ya Bambino Gesù ametembelea idara ya huduma
kwa watoto mahututi waliofanyiwa upasuaji wa moyo; sehemu ambayo hivi karibuni ilifanyiwa
ukarabati mkubwa, ili kuiwezesha Hospitali kutoa huduma makini kwa watoto wanaotoka
sehemu mbali mbali za dunia. Itakumbukwa kwamba, hata watoto kutoka Tanzania kwa miaka
kadhaa walikuwa wanapata tiba ya magonjwa ya moyo kwa kushirikiana na Hospitali ya
Mtakatifu Gaspar, iliyoko Itigi, Singida, Tanzania.
Baadaye Kardinali Parolin
amepata fursa ya kukutana na kuzungumza na wagonjwa, wafanyakazi na watu wanaojitolea
kutoa huduma mbali mbali hospitalini hapo na kuwashukuru kwa moyo wao wa upendo, ukarimu
na mshikamano, uliowezesha Hospitali ya Bambino Gesù kutoa huduma kwa familia 4500,
karibu ya watu 13, 500 pamoja na huduma kwa watu zaidi ya 102, 000 waliohudumiwa katika
majengo ya Hospitali ya Bambino Gesù.
Kardinali Parolin amewashukuru na kuwapongeza
kwa kazi kubwa wanayoitekeleza kwa niaba ya Mama Kanisa miongoni mwa watoto wadogo,
kwa kuwaonjesha upendo, ukarimu na mshikamano mambo muhimu yanayousukuma ulimwengu
kusonga mbele kwa imani na matumaini, licha ya mapungufu ya kibinadamu. Huduma zinazotolewa
Hospitalini hapo zinawawezesha wazazi na watoto wagonjwa kuishi katika mazingira bora
yanayoheshimu na kujali utu wa binadamu, changamoto ya kuendelea kuwamegea watu upendo
huu siku kwa siku. Kardinali Parolin anasema, huu ndio ujumbe na matashi mema ya Noeli
kwa Mwaka 2014.
Kardinali Parolin ametembelea na kusali kidogo kwenye Kikanisa
cha Hospitali ya Bambino Gesù kilichojengwa kunako mwaka 1869 na Familia ya Salviati
waliotoa zawadi kwa Vatican kunako mwaka 1924. Kikanisa hiki kinahifadhi masalia ya
Watakatifu Yohane XXIII na Yohane Paulo II. Kabla ya kurejea mjini Vatican, Kardinali
Parolin amewatembelea wagonjwa waliolazwa kwenye wodi ya mfumo wa chakula, eneo ambalo
pia linatoa huduma kwa wagonjwa wenye magonjwa nasibu.