Baraza la Makanisa Ulimwenguni linapenda kuendeleza hija ya kiekumene kwa kuwa na
mwelekeo mpya, huku likijitahidi kutumia fursa mbali mbali zinazojitokeza, ili kumwilisha
dhana hii katika uhalisia wa maisha na utume wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, kwa
kuongozwa na kauli mbiu “hija ya haki na amani, mwono uliotolewa kwenye mkutano mkuu
wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni ulioadhimishwa Korea ya Kusini, Desemba 2013.
Akitafakari
kuhusu changamoto hii, Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni
anasema, Makanisa Ulimwenguni hayana budi kusonga mbele kwani dunia inaendelea kucharuka,
kwa kusoma alama za nyakati pamoja na kutumia fursa mbali mbali zinazojitokeza, ili
kuwaendea wale walioko pembezoni mwa jamii. Baraza la Makanisa Ulimwenguni halina
budi kuendelea kujikita katika mchakato wa kuimarisha umoja na mshikamano na Makanisa
mbali mbali, ili kuwatangazia vijana wa kizazi kipya Habari Njema ya Wokovu.
Dr.
Tveit ameyasema haya hivi karibuni alipokuwa anazungumza kwenye Mkutano wa Kamati
kuu ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni, iliyokutana huko Paralimni, Cyprus. Kamati
kuu imefanya mkutano huu nchini Cyprus, mahali ambapo watu wengi wanaendelea kuteseka
kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa. Ni watu wanaohitaji kuonjeshwa moyo
wa upendo na mshikamano, bila kuwasahau Wakristo wanaoendelea kunyanyaswa na kudhulumiwa
sehemu mbali mbali za dunia kutokana na imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.
Umoja
na mshikamano ni nyenzo muhimu sana katika kuwahudumiwa walimwengu pamoja na kujibu
kilio cha watu wote wanaoteseka kutokana na ukosefu wa misingi ya haki, amani na utulivu.
Umoja na mshikamano wa kiimani ni ushuhuda mkubwa wenye mvuto na mashiko kwa watu
wengi duniani. Cyprus ni kitovu cha mshikamano na wahamiaji pamoja na wageni wanaotafuta
nafuu ya maisha Barani Ulaya.
Baraza la Makanisa Ulimwenguni katika mpango
kazi wake, linapania kuendelea kuhimiza misingi ya haki na amani huko Syria, Iraq,
Ukraine, Korea ya Kusini na Kaskazini; Israeli na Palestina, Nigeria, Sudan ya Kusini
na huko DRC. Hizi ni nchi ambazo zinahitaji kwa namna ya pekee amani na utulivu. Baraza
la Makanisa Ulimwenguni linaendelea kuhamasisha umuhimu wa jamii za watu kuzingatia
misingi ya haki, amani na maendeleo endelevu. Baraza la Makanisa pia linapenda kusimama
kidete kuchangia katika dhana ya utunzaji bora wa mazingira, kwa kushirikisha Umoja
wa Mataifa, mawazo na changamoto zao.
Baraza la Makanisa Ulimwengu litaendelea
kushirikiana na wadau mbali mbali katika mchakato wa maendeleo endelevu ya binadamu;
utoaji wa msaada wa dharura, kusimamia haki msingi za binadamu pamoja na kuhakikisha
kwamba, kunakuwepo na haki sawa katika masuala ya tabianchi, bila kusahau mchango
wa Makanisa katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi na Ebola ambao kwa sasa limekuwa
ni janga la kimataifa.
Baraza la Makanisa Ulimwenguni litaendelea kukuza na
kudumisha umoja na Kanisa Katoliki, ambalo kimsingi si mwanachama wa Baraza hili,
lakini limekuwa likishiriki kikamilifu katika mikutano na mikakati yake.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.