Padre Raniero Cantalamessa, mhubiri mkuu wa nyumba ya kipapa, kuanzia Ijumaa ya tarehe
5 Desemba 2014 ataanza kutoa mahubiri ya kipindi cha Majilio kwa Baba Mtakatifu Francisko
na viongozi wengine wa Kanisa wanaoishi mjini Roma. Mwaka huu, Padre Cantalamessa
anasema, mahubiri yake yatajikita katika “Amani na Mwenyezi Mungu ndiyo inayojenga
mahusiano mema ya kibinadamu”.
Mahubiri haya
yatatolewa kwenye Kikanisa cha Mama wa Mkombozi, kilichoko mjini Vatican. Mahubiri
haya yataongozwa kutoka katika Injili kama ilivyoandikwa na Luka, sura ya 2: 14 “Atukuzwe
Mungu juu mbinguni na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia”. Hii ni tema muhimu
sana kwa wakati huu ambako mtutu wa bunduki unaendelea kurindima sehemu mbali mbali
za dunia na kusahau kwamba, amani ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayomwajibisha
binadamu.
Umefika wakati kutoa maana ya kina ya neno “Amani” na baadaye kuendelea
kusikiliza ujumbe wa kuzaliwa kwa Mkombozi na Mfalme wa amani duniani, huku waamini
wakiwa na mwelekeo mpya wa maisha, tayari kumwilisha ujumbe wa siku ya kuombea amani
duniani, inayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe Mosi, Januari, sanjari na Siku
kuu ya Bikira Maria Mama wa Mungu, “Theotokos” kama inavyojulikana tangu awali na
Mababa wa Kanisa.
Ijumaa ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, Padre Cantalamessa
anasema kwamba, atafanya tafakari ya kina kuhusu amani kama zawadi kutoka kwa Yesu
Kristo, zawadi ambayo Mwenyezi Mungu anamkirimia mwanadamu, hali inayojionesha katika
kazi ya Uumbaji.
Pale mwanadamu anapojitahidi kujenga na kudumisha amani na
Mwenyezi Mungu anaweza kupata pia amani ndani mwake na kati ya watu wanaomzunguka;
amani inadumishwa kati ya binadamu na mazingira yake. Lakini, kunapatashika nguo kuchanika,
ikiwa kama mwanadamu atashindwa kujenga na kudumisha amani na Mwenyezi Mungu, matokeo
yake ni kinzani kati ya Adamu na Eva, kati ya mtu na mtu na haya ndiyo yanayosimuliwa
kwenye Kitabu cha Mwanzo.
Mwanadamu anaweza kuweka sahihi ya mkataba wa amani,
lakini hakupatikani na amani ya kweli, hadi pale mahusiano ya dhati yatakapojengwa
na Mwenyezi Mungu, matokeo yake ni watu daima kupenda kurudi msituni! Amani ya kweli
inajikita kwa kutambua ukuu na wema wa Mungu katika maisha ya mwanadamu.
Kwa
waamini anasema Padre Cantalamessa, amani hii inapata chimbuko lake kutoka katika
Fumbo la Utatu Mtakatifu, changamoto ya kujenga na kudumisha umoja, udugu na mshikamano
kati ya watu. Mahusiano haya ni muhimu hata katika mahusiano ya kitamaduni kwa watu
mamboleo, vinginevyo, watu wataogelea katika utupu, kinzani na migongano ya kivita.
Ijumaa
ya Pili ya Kipindi cha Majilio, tarehe 12 Desemba 2014: Tafakari itajikita katika
Amani kama wajibu na dhamana inayopaswa kufanyiwa kazi. Hapa waamini wanaalikwa kujichotea
utajiri kutoka katika muhtasari wa Mafundisho makuu ya Yesu, juu ya Heri za Mlimani,
yaani … Heri wapatanishi. Hapa Padre Cantalamessa anasema, halengi kuzungumzia masuala
ya kisiasa kwani huu kwa sasa ni wimbo usiokuwa na kiitikio.
Hapa mkazo ni
kuona jinsi gani Yesu alivyowafundisha Wafuasi wake kupata amani ya kweli na inayodumu.
Ni wakati wa kuangalia umuhimu wa dini mbali mbali kujenga na kudumisha misingi ya
amani, kwa kukazia amani na majirani bila kusahau kwamba, hata Watoto wa Kanisa wanapaswa
kutawaliwa na misingi ya amani, kwa kujenga na kukuza umoja, mshikamano na udugu ndani
ya Kanisa.
Ijumaa ya tatu ya Kipindi cha Majilio: tarehe 19 Desemba 2014, tafakari
itajikita katika amani kama zawadi kutoka kwa Roho Mtakatifu, anayemwezesha mwamini
kupata utulivu wa ndani. Padre Cantalamessa anasema, mahubiri ya Kipindi cha Majilio
yanalenga kwa namna ya pekee kuwasaidia viongozi wa Kanisa katika safari ya maisha
yao ya kiroho, ili kuwajalia kuwa na amani na utulivu wanapotekeleza dhamana na majukumu
yao ya kila siku. Amani ya kweli inapatikana kwa kutekeleza mapenzi ya Mungu.
Na
Padre Richard A. Mjigwa, Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.