Uingereza na Vatican kwa pamoja zinataka kulinda na kudumisha amani, majadiliano na
upatanisho!
Yesu Kristo anaendelea kuwaita na kuwatuma wafuasi wake kwenda sehemu mbali mbali
za dunia ili kupeleka Habari Njema ya Wokovu inayojisimika katika misingi ya haki,
amani na upatanisho, changamoto na mwaliko kwa Uingereza na Vatican kushirikiana kwa
pamoja katika kuimarisha tunu hizi msingi kwa ajili ya mafao na ustawi wa wengi.
Hii
ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican,
Jumatano tarehe 3 Desemba 2014 wakati wa maadhimisho ya kumbu kumbu ya Karne moja,
tangu Uingereza na Vatican ziliporudisha tena mahusiano ya kidiplomasia. Ibada hii
imefanyika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Paulo, nje ya kuta za Roma na kuhudhuriwa
na viongozi wa Kanisa na Serikali kutoka Uingereza na Vatican.
Kardinali Parolin
katika mahubiri yake amezitaka nchi hizi mbili kuendelea kushirikiana kwa dhati ili
kulinda na kutetea wanyonge kama ilivyokuwa wakati wa Vita kuu ya kwanza na ya Pili
ya Dunia na kama hali inavyojionesha kwa sasa. Wawe ni wadau wakuu katika kuhamasisha
mchakato wa majadiliano ya upatanisho kati ya watu, ili kujenga na kuimarisha haki
na amani miongoni mwa jamii ya binadamu pamoja na kuendelea kutoa msaada wa hali na
mali kwa watu wanaokumbwa na maafa na majanga asilia sehemu mbali mbali za dunia.
Hii ni changamoto pia ya kukumbatia na kuenzi Injili ya Uhai kwa kutetea zawadi
ya maisha tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida
inapomfika kadiri ya mpango wa Mungu pamoja na kukataa kishawishi cha kutaka kukumbatia
utamaduni wa kifo unaojikita katika sera za kifo laini, biashara haramu ya binadamu
pamoja na kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu.
Kardinali
Parolin amepongeza juhudi zinazofanywa na nchi hizi mbili kwa kuzingatia tunu msingi
za maisha ya Kikristo na kimaadili sanjari na mchakato wa majadiliano ya kiekumene
unaotekelezwa na Baraza la Kipapa la uhamasishaji wa umoja wa Wakristo, ingawa bado
kuna madonda makubwa ya utengano huu yanayoapaswa kufanyiwa kazi, ili kupata tiba
muafaka.
Kardinali Parolin anasema, maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwa
ajili ya kumshukuru Mungu kwa kipindi cha Karne moja tangu Vatican na Uingereza viliporudisha
mahusiano ya kidiplomasia ni kielelezo kwamba, imani imekuwa ni msingi katika mchakato
wa majadiliano baina ya pande hizi mbili. Wakristo bado wanahamasishwa kutoka kifua
mbele kwenda ulimwenguni ili kuwatangazia Watu wa Mataifa Habari Njema ya Wokovu;
dhamana inayowahitaji watu wanaojisadaka kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake.
Waamini
wajitahidi kusoma, kulisikiliza, kulitafakari na hatimaye kulimwilisha Neno la Mungu,
ilikuzima njaa na kiu ya Neno la Mungu katika maisha ya watu. Watu wana kiu ya ukweli
na upendo unaobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Kardinali Parolin amekumbusha
kwamba, katika kipindi cha miaka mingi kupita, Mtakatifu Yohane Paulo II kunako mwaka
1982 alithubutu kutembelea Uingereza na baadaye, Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto
XVI alipokwenda Uingereza ili kumtangaza Kardinali John Henry Newman kuwa Mwenyeheri.
Malkia Elizabeth wa Uingereza alimtembelea Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican
tarehe 3 Aprili 2014.
Uhusiano wa kidiplomasia kati ya Vatican na Uingereza
uliingiwa na mchanga kwa muda wa miaka 340 hadi ilipogota tarehe 7 Desemba 1914, nchi
hizi mbili zikarudisha tena uhusiano wao wa kidiplomasia. Kweli ni rahisi kuvuruga
mahusiano ya kidiplomasia, lakini kuyarudisha tena, itachukua miaka mingi.
Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.