2014-12-04 10:58:11

Mikakati ya maendeleo itoe kipaumbele cha kwanza katika kupambana na umaskini, njaa na lishe duni!


Umoja wa Mataifa ni jukwaa ambalo watu wasiokuwa na sauti wanaweza kusikilizwa kwa heshima na taadhima, ili kuibua mbinu mkakati utakaofanyiwa kazi na Jumuiya ya Kimataifa mara baada ya kukamilika kwa Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015.

Mikakati ya maendeleo itakayofuatia, haina budi kupata ridhaa ya wanachama wengi kutoka Jumuiya ya Kimataifa, bila shuruti ya aina yoyote ile na kwamba, kuna haja ya kutafuta ushauri mpana zaidi, ili kweli Jumuiya ya Kimataifa iweze kupata mafanikio makubwa zaidi katika mikakati ya maendeleo endelevu. Hapa kuna haja ya kufanya upembuzi yakinifu kwa kupima mafanikio, matatizo na changamoto zitakazokuwa zinajitokeza katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo baada ya mwaka 2015.

Ni changamoto ambayo imetolewa na Askofu mkuu Bernadito Auza, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa, wakati akichangia hoja kwenye kikao cha sitini na tisa cha Baraza kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu mikakati ya maendeleo mara baada ya mwaka 2015. Anasema vielelezo vinavyotolewa havina budi kuchambuliwa kwa umakini mkubwa ili kuangalia kama vinatekelezeka kutokana na utofauti mkubwa unaojionesha kati ya nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa.

Askofu mkuu Auza anasema, kipaumbele cha kwanza kiwe ni kupambana na umaskini, baa la njaa na utapiamlo mambo ambayo bado yanasababisha majanga makubwa kwa wananchi wengi wanaoishi katika Nchi zinazoendelea duniani, kwani huu ni wajibu wa kimaadili kutoka katika Jumuiya ya Kimataifa kama alivyokazia Baba Mtakatifu Francisko alipokuwa anazungumza na wajumbe wa mkutano wa FAO hivi karibuni mjini Roma.

Utekelezaji wa mikakati hii uwe ni mwendelezo wa mafanikio yaliyopatikana siku za nyuma, kwa kuweka masuala ya ushauri katika mfuko wa maendeleo wakati ambapo mikakati ya maendeleo endelevu iunganishwe katika masuala ya mabadiliko ya tabianchi. Ujumbe wa Vatican unatarajia kuendelea kushiriki kikamilifu katika mikutano mikuu itakayofanyika hapo mwakani pamoja na ule unaotarajiwa kuwakutanisha wakuu wa Nchi na Serikali mwezi Septemba, 2015.







All the contents on this site are copyrighted ©.