2014-12-04 09:10:06

Mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu!


Jeshi la Polisi na Kanisa ni wadau wakuu katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu inayoendelea kunyanyasa na kufisha utu na heshima ya binadamu. Biashara hii haramu ni kati ya majanga makubwa yanayomwandama mwanadamu katika ulimwengu mamboleo na kwamba, huu ni uhalifu dhidi ya binadamu.

Kwa muda wa siku mbili, kuanzia tarehe 5 hadi tarehe 6 Desemba, 2014 mjini London, Uingereza kunafanyika mkutano wa kimataifa dhidi ya biashara haramu ya binadamu ulioandaliwa na Kikundi cha Santa Marta kwa kushirikiana na Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza na Jeshi la Polisi nchini Uingereza. Viongozi mbali mbali wa Kanisa na Serikali ya Uingereza wanatarajiwa kushiriki katika mapambano haya dhidi ya biashara haramu ya binadamu.

Kikundi cha Santa Marta kilichoanzishwa kunako mwezi Aprili 2014 kinaongozwa na Bwana Bernard Hogan-Howe pamoja na Kardinali Vincent Nichols, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza na Wales, kwa kushirikiana na wakuu wa Majeshi ya Polisi na Maaskofu kutoka sehemu mbali mbali za dunia; wanaofanya kazi kwa pamoja ili kung'oa biashara haramu ya binadamu pamoja na kutoa huduma za kichungaji kwa wahanga wa vitendo hivi kwa kinyama.

Kikundi hiki kinapania pamoja na mambo mengine, kuibua mbinu mkakati wa kuzuia, huduma za kichungaji pamoja na kushirikiana kimataifa katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu.







All the contents on this site are copyrighted ©.