2014-12-03 08:44:04

Taalimungu iguse imani na maisha ya Watu wa Mungu!


Taalimungu ya kina inapata chimbuko lake katika maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa, katika Ibada ya kuabudu Fumbo la Utatu Mtakatifu na kwa namna ya pekee kwa kutafakari Neno wa Mungu aliyefanyika mwili. Mafumbo ya Imani hayana budi kugusa akili, utashi na maisha ya wale wote wanaojitaabisha kutafuta elimu juu ya Mwenyezi Mungu, daima wakiomba msada wa neema ya Roho Mtakatifu, ili aweze kuimarisha utashi wa binadamu katika kuyatafakari matendo ya Mungu katika maisha ya mwanadamu.

Hii ni changamoto ambayo imetolewa na Kardinali Gerhard Ludwig Mùller, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa na Rais wa Tume ya Kitaalimungu Kimataifa, iliyoanza mkutano wake wa Mwaka mjini Vatican tarehe Mosi, Desemba 2014.

Kardinali Mùller anawataka wajumbe wa Tume hii kuhakikisha kwamba, wanatumia vyema akili na utashi wao, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa, kwani huu ni wito maalum kabisa wanaopaswa kuutekeleza wakitambua kwamba, wana dhamana kubwa katika maisha na utume wa Kanisa. Wanataalimungu wanatakiwa kuwa tayari siku zote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yao, kama anavyosema Mtakatifu Petro.

Taalimungu inafanya upembuzi yakinifu kwa kujikita katika imani, utulivu na ukweli katika imani; mambo msingi yanayopania kujenga msingi wa ufunuo wa Mwenyezi Mungu, mmoja katika Fumbo la Utatu Mtakatifu. Hili ni Fumbo la Mungu linalojidhihirisha kwa namna ya pekee katika historia ya ukombozi na kilele chake ni Neno wa Mungu kufanyika mwili na hivyo kuweza kueleweka hata katika akili ya binadamu.

Taalimungu haina budi kujikita katika maisha ya waamini, akili na uhalisia wa maisha unaojidhihirisha katika maadhimisho mbali mbali kwa lengo la kupata dira na mwelekeo wa shughuli za kichungaji. Taalimungu anasema Kardinali Mùller haina budi kuwa ni kielelezo cha imani katika matendo na maisha ya waamini, kama ambavyo Fumbo la Utatu Mtakatifu linavyodhihirisha umoja. Huu ndio msingi wa Uinjilishaji unaotekelezwa na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Yesu Kristo ni mwanataalimungu wa kwanza hata kabla ya Maandiko Matakatifu na anajionesha kwa wafuasi wake kuwa ni njia, ukweli na uzima na kwamba, hakuna ukweli pasi na maisha na wala maisha pasi na ukweli. Kwa njia ya Yesu Kristo, wanataalimungu wanaweza kuufahamu ukweli uliojisadaka na kuwa ni sehemu ya maisha kwa wafuasi wake.

Tume ya kitaalimungu kimataifa inatekeleza wajibu na utume wake kwa njia ya mshikamano wa kijumuiya na kidugu, kwa kuheshimiana, kushirikiana na ugudu, ili kukuza na kudumisha majadiliano ya kweli sanjari na kuheshimu Mafundisho ya Kanisa pamoja na kuwajibika barabara mbele ya Khalifa wa Mtakatifu Petro aliyepewa dhamana ya kuliongoza Kanisa la Kristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.