2014-12-03 11:09:37

Nendeni Jangwani mkakutane na Mungu!


Tuangalie kwa kifupi masomo yetu yatuambia nini leo: Katika somo la kwanza twaona tangazo la ukombozi kwa Waisraeli na wito wa kurudi kutoka utumwani. Je nasi pia tuko utumwani? Mungu yupo – tuutafute wokovu, maadam unapatikana. Katika somo la pili – anayekesha mara nyingi aweza kuona siku zinakawia. Bali Bwana atupa sisi nafasi ya kukiri dhambi, kutubu na kumwongokea.

Katika Injili – twaona kuwa ujio ya Yesu Kristo unatayarishwa au kuonekana na Nabii muungamaji. Kwa mfano wake wa maisha na Neno lake – mioyo ya watu imepata kuandaliwa kwa ujio wa Bwana. Yohane anawaita watu watoke, waonekane katika uwazi, ili Mungu awapate. Waisraeli walikutana na Mungu jangwani, waliacha yote, walikuwa watupu – Mungu akapata nafasi ya kuwaita.

Mhubiri maarufu Munachi anaanza mahubiri yake jumapili hii ya leo akitoa mfano huu ;
Mfano wa mtoto na mgeni;
Mgeni anaenda nyumbani kwake na kuuliza - Baba yupo?
Jibu la mtoto – ndiyo.
Mgeni- naweza kuongea naye.
Mtoto anajibu kwa sauti ndogo kabisa - hapana.

Mgeni anaendelea - Mama yupo?
Mtoto– ndiyo. Lakini pia mtoto anaendelea kumjibu mgeni kuwa hawezi kuonana naye. Mgeni anaendelea – Je, yupo mtu mwingine yeyote ninayeweza kuongea naye?
Mtoto anajibu - ndiyo yupo Polisi.

Mgeni anataka kuongea naye? Mtoto anajibu hapana kwa vile anaongea na mzima moto. Mgeni anauliza - ulizuka moto? Mtoto anajibu hapana ila wananitafuta. Hakika katika mazingira kama haya yaonekana wazi kuwa mtoto huyu amejificha na anatafutwa na wazazi wake. Asipotoka nje na kuonekana hakika hatapatikana. Ndicho kinachoonekana leo katika masomo yetu na tafakari yetu ya leo. Mungu yupo amejionesha, anatutafuta na anataka tukutane naye. Ila pengine mazingira yetu hayatoi nafasi ili kukutana naye.

Katika Biblia - Jangwa laonesha sehemu iliyo wazi, panapoonekana. Haja ya kutoka nje ni muhimu, ni lazima wahusika watoke nje ili waonekane. Leo Yohane Mbatizaji aliyeishi alichofundisha anaenda Jangwani. Sote twaitwa tutoke ndani yetu tuende nje, tuende kukutana na Mungu. Mwaliko wa kujuta na kuungama dhambi zetu huku tukimngojea huyo ajaye tukiwa tuko tayari. Ni kipindi cha kutambua mahitaji yetu ya Mungu.

Kipindi cha majilio ni kipindi cha kumbukumbu na matumaini. Mtakatifu Augustino, Askofu na Mwalimu wa Kanisa anasema, Mungu ametuumba sisi kwa ajili yake. Na ametuumba bila hiari yetu ila kuupata wokovu ni juhudi binafsi. Na anaendelea kusema - mioyo yetu haitatulia ila kwa Bwana. Hivyo wito wa kutoka ndani na kwenda nje uko wazi hapa. Yohane Mbatizaji amefanya hilo na akawavuta watu. Kinachotakiwa hapa ni uongofu toka ndani - metanoia. Mtakatifu Yohane atuita na anafanya jambo - yeye anaenda jangwani anafanya anachosema na watu wanamfuata wanapata wanachohitaji.

Wito wetu leo tuwe mwanzo wa Injili, yaani watangazaji wa habari njema. Tuangalie mahitaji yetu ya leo na mahitaji ya ulimwengu wetu wa leo? Ili hiyo habari njema iseme zaidi miongoni mwa watu? Yesu ndiye kamisaa, Yohane mbatizaji mwamuzi wa Mpira na sisi washika vibendera - tuko pamoja au tumeangalia vitu vingine tu? Ubinafsi wetu tu?

Mwinjili Marko anaanza injili akitangaza uwepo wa Mungu kati yetu - sisi tunaalikwa kuwa wajumbe wa uwepo wa Mungu hapa duniani. Kipindi cha majilio kimewekwa ili tuweze kumwona tena Yesu kati yetu. Mfano wa mpiga Zumari maarufu – Paganini -ni baada ya kupiga muziki kwa muda mrefu anagundua baadaye sana kuwa mpiga muziki ni yeye na si kile chombo anachotumia. Muziki unatoka ndani yake na si katika chombo. Chombo chatumika kama kifaa tuu. Hivyo nasi pia hatuna budi kutambua haja ya kuwa wachezaji wa mchezo, watangazaji wa hiyo Habari Njema na si kinyume chake.

Tumsifu Yesu Kristo.
Imeandaliwa na Pd. Reginald Mrosso, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.