Australia itaendelea kushirikiana na Kanisa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi!
Askofu mkuu Dominique Mamberti aliyekuwa Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano
wa kimataifa mjini Vatican, amehitimisha safari ya kikazi nchini Australia kama kilele
cha maadhimisho ya Karne moja tangu nchi hii ilipopandishwa hadhi na kuwa ni sehemu
ya utume wa Kanisa na miaka arobaini ya uhusiano wa kidiplomasia kati ya Australia
na Vatican.
Akiwa nchini Australia, Askofu mkuu Mamberti amepata fursa ya
kukutana na kuzungumza na viongozi wa Kanisa na Serikali pamoja na kushirikishana
mambo msingi yaliyojiri wakati wa mkutano wa viongozi wakuu wa G20 uliofanyika hivi
karibuni nchini Australia. Wameshirikisha yale yanayoendelea huko Mashariki ya Kati:
mchango wa Kanisa Katoliki na majadiliano yanayoendelea huko katika mchakato wa kutafuta
haki, amani na utulivu.
Wakati huu Mama Kanisa anapojiandaa kwa ajili ya maadhimisho
ya awamu ya pili ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu familia, Askofu mkuu Mamberti pamoja
na wenyeji wake wamejadiliana kwa kina na mapana dhamana na utume wa familia. Wamekazia
umuhimu wa watu kushirikishwa kikamilifu katika maisha ya jamii inayowazunguka.
Akiwa
nchini Australia, Askofu mkuu Mamberti amepata nafasi ya kuadhimisha Fumbo la Ekaristi
Takatifu na kutoa Sakramenti ya Kipaimara, kwa kuwataka vijana kuwa ni mashahidi wa
Yesu Kristo na Kanisa lake ndani ya familia na sehemu mbali mbali za maisha yao. Ametembelea
na kusali kwenye kaburi la Mtakatifu Mary MacKillop, mwamini wa kwanza kutoka Australia
kutangazwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI kuwa Mtakatifu. Amepewa pia shahada
ya heshima katika masuala ya kidiplomasia, tukio lililomwezesha kupembua kwa kina
na mapana kuhusu mchango wa Kanisa Katoliki katika ustawi na maendeleo ya watu kwa
kuwashukuru wote waliochangia kwa hali na mali.
Askofu mkuu Dominique Mamberti
akizungumza na Maaskofu wa Australia, amejikita katika utume na dhamana inayotekelezwa
na wanadiplomasia wa Vatican sehemu mbali mbali za dunia; hali tete huko Mashariki
ya Kati na kwamba, Baraza la Maaskofu Katoliki Australia, Jumapili tarehe 7 Desemba
2014 wataadhimisha Siku ya Mshikamano na Wakristo Mashariki ya Kati na kwamba, ujumbe
wa Baraza la Maaskofu Katoliki Australia utatembelea Iraq na Lebanon ili kuwatia shime
Wakristo huko Mashariki ya Kati.
Askofu mkuu Mamberti alipata fursa ya kuzungumza
na viongozi wakuu wa Serikali ya Australia kwa kujikita zaidi katika vitendo vya kigaidi
na mambo ambayo yanapelekea vijana wengi kujiunga na vitendo hivi vya kigaidi kiasi
cha kutoogopa kufa; shida na mahangaiko ya Wakristo huko Mashariki ya Kati; Majadiliano
ya kidini na kiekumene nchini Australia; nyanyaso za wanawake na wasichana sehemu
mbali mbali za dunia pamoja na mchango wa Serikali ya Australia kwa kushirikiana na
Caritas Australia.
Askofu mkuu Mamberti ametembelea Makumbusho ya Kale na Kumbu
kumbu za Vita kuu ya Pili ya Dunia, kwa kuangalia picha za watu waliojisadaka kwa
ajili ya nchi yao. Ameadhimisha pia Siku kuu ya Papa kwa kumshukuru na kumpongeza
Askofu mkuu Paul Richard Gallagher, aliyeteuliwa hivi karibuni na Baba Mtakatifu Francisko
kuwa Katibu mkuu wa Mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican,
anatarajiwa kuanza utume waka rasmi, mwezi Januari, 2015. Vatican itaendelea kujielekeza
zaidi katika mchakato wa kutafuta haki, amani, ustawi na maendeleo ya wengi.
Askofu
mkuu Dominique Mamberti, kabla ya kurejea mjini Roma, ametembelea Chuo kikuu cha Kikatoliki
nchini Australia, kwa kuwataka wadau kuhakikisha kwamba, wanasaidia kukoleza mchakato
wa majiundo makini ya wanafunzi: kiroho, kimwili, kimaadili, kiutu na kitaaluma. Australia
na Vatican katika kipindi cha miaka arobaini wameimarisha uhusiano wao wa kidiplomasia,
kwa ajili ya mafao ya pande hizi mbili.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.