2014-12-02 14:41:29

Mtu mnyenyekevu anauwezo wa kumfahamu Mungu na taalimungu inafanyika kwa njia ya sala na tafakari!


Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican, Jumanne, tarehe 2 Desemba 2014 amewataka wale wote wanaojifunza taalimungu, kuifanya shughuli hii kwa kupiga magoti, moyo mkuu na unyenyekevu, kwani imependeza Mwenyezi Mungu kujifunua kwa watu wanyenyekevu kama walivyo watoto wadogo, na kamwe wasitegemea akili zao wenyewe, vinginevyo watashindwa kulifahamu Fumbo la Maisha ya Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu anasema, Ufalme wa Mungu ulioanzishwa na Yesu Kristo mwenyewe ni kwa ajili ya maskini wa roho kama anavyofundisha Mwinjili Luka, ndiyo maana Yesu anamshukuru Baba yake wa mbinguni kwa kuyaficha mambo haya na kuwafunulia watoto wadogo, kwani ndivyo ilivyompendeza, mwaliko kwa Wakristo kujenga na kukuza moyo wa unyenyekevu, kwa njia ya sala na tafakari ya kina.

Umaskini wa roho ni udongo mzuri kwa ajili ya kutafakari Fumbo la Utatu Mtakatifu. Yesu anajifunua si kama nahodha, kiongozi mwenye nguvu na madaraka makubwa au jemedari wa vita bali kama mche mwororo, mpole na mnyenyekevu wa moyo. Yesu anakuja kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti, ili kumshirikisha ile furaha ya uzima wa milele. Anakuja kuwatangazia Habari Njema ya Wokovu, wagonjwa, maskini na wale wote wanaodhulumiwa na kunyanyaswa.

Ukuu wa Fumbo la Maisha ya Mungu unaweza kufahamika anasema Baba Mtakatifu kwa njia ya Yesu Kristo, aliyejinyenyekesha, hata kufa Msalabani, nje ya Yesu ni vigumu sana kuweza kumfahamu Mwenyezi Mungu. Kipindi cha Majilio, iwe ni fursa kwa waamini kumkaribia zaidi Mwenyezi Mungu na kutembea pamoja naye katika hali ya unyenyekevu, upole na umaskini, kwa kujisikia kuwa ni wadhambi wanaohitaji kuonja huruma na upendo kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Yesu anakuja ili kumkomboa mwanadamu!







All the contents on this site are copyrighted ©.