Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa, Rehema kamili kutolewa kwa waamini!
Katika maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani, unaowachangamotisha watawa wa Mashirika
ya Kitawa na Kazi za Kitume kuyapyaisha tena maisha na utume wao ndani ya Kanisa,
kwa kuendelea kuwa waaminifu kwa karama za waanzilishi wa Mashirika yao pamoja na
kutoa fursa kwa Familia yote ya Mungu kuweza kufurahia maadhimisho haya katika imani,
matumaini na mapendo huku wakiungana na Kanisa zima, Baba Mtakatifu Francisko ametoa
zawadi ya rehema kamili kwa waamini wote watakaotimiza masharti yaliyowekwa.
Ili kupata
rehema kamili, mwamini atapaswa kupokea Sakramenti ya Upatanisho, Ekaristi Takatifu
na kusali kwa ajili ya nia za Baba Mtakatifu. Zawadi hii inatolewa kwa waamini wote
watakaotekeleza masharti haya tangu Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Majilio, hadi
tarehe 2 Februari 2016, Kanisa litakapokuwa linafunga rasmi Mwaka wa Watawa Duniani.
Rehema
kamili itatolewa pia kwa waamini watakaosali kwa ajili ya kuombea roho za waamini
marehemu, kila wakati watakapokuwa wanashiriki katika matukio mbali mbali ya kimataifa
yatakayofanyika mjini Roma kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani;
kwa kusali sala ya Baba Yetu, Kukiri Kanuni ya Imani pamoja na kusali Sala zilizokubaliwa
na Kanisa kwa Bikira Maria.
Rehema kamili pia itatolewa kwa wale wote watakaotembelea
kwenye Makanisa mahalia, nyumba za kitawa au madhabahu maalum yaliyotengwa wakati
wa Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani na kusali Sala ya Kanisa hadharani au ibada
nyingine na kuhitimisha kwa kusali Sala ya Baba Yetu, Kukiri Kanuni ya Imani na kumwomba
Bikira Maria.
Rehema kamili itatolewa pia kwa watawa ambao kutokana na ugonjwa
au sababu mbali mbali watashindwa kuhudhuria katika maeneo yaliyotengwa, kwa kujitenga
na dhambi na kunuia kutekeleza mapema iwezekanvyo masharti yaliyotajwa, kwa kufanya
hija ya kiroho huku wakitolea mateso na mahangaiko yao kwa Mwenyezi Mungu, mwingi
wa huruma na mapendo kwa njia ya Bikira Maria na kusali kama inavyotakiwa.
Huu
ni mwaliko kwa Mapadre kuhakikisha kwamba, wanatoa nafasi kwa waamini wanaokimbilia
huruma ya Mungu kwa njia ya Sakramenti ya Upatanisho; Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi
Takatifu pamoja na Mpako Mtakatifu kwa ajili ya wagonjwa. Waamini wataweza kupata
rehema kamili wakati wote wa Maadhimisho ya Mwaka wa Watawa Duniani.
Na Padre
Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.