Kanisa linapania kutangaza Injili ya Familia kwa Watu wa Mataifa!
Askofu mkuu Joseph Edward Kurtz, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani anasema
kwamba, maadhimisho ya Sinodi maalum ya Maaskofu kwa ajili ya Familia yalisimikwa
katika mambo makuu mawili, mang’amuzi na uamuzi wa pamoja na kwamba, Mababa wa Sinodi
walijitahidi kujadili mambo yote katika ukweli na uwazi, ili kuliwezesha Kanisa kuendelea
kutangaza Injili ya Familia.
Askofu mkuu
Kurtz akizungumzia kuhusu ushiriki wa vyombo vya habari anasema, hii ni Sinodi iliyolenga
kuwasaidia Mababa wa Sinodi kusikiliza kwa makini kuhusu changamoto zinazoendelea
kujitokeza katika maisha na utume wa Kanisa kuhusiana na Familia. Hati ya Mababa wa
Sinodi inaonesha mwanzo wa safari kubwa ambayo inawasubiri Mababa wa Kanisa, changamoto
kwa Familia ya Mungu kuanza kuifanyia kazi kwa ajili ya maadhimisho ya kawaida ya
Sinodi ya Maaskofu kuanzia tarehe 4 Oktoba 2015 hadi tarehe 25 Oktoba 2015.
Askofu
mkuu Kurtz anasema, Mababa wa Sinodi katika majadiliano yao, hawakuonesha nia ya kutaka
kupingana na Mafundisho tanzu ya Kanisa kuhusu maisha ya ndoa na familia, bali kusoma
alama za nyakati, ili kuweza kuzisaidia familia kutekeleza dhamana na wajibu wake
barabara. Anasema, Hati elekezi ambayo ilikuwa ni mkusanyiko wa mchango wa Mababa
wa Sinodi, ilionesha vipengele ambavyo vilitibua nyongo za baadhi ya waamini sehemu
mbali mbali duniani, lakini wengi walisahau kwamba, haya yalikuwa ni mawazo tu na
wala hakuna maamuzi ambayo yalikuwa yamefikiwa.
Kwa maneno mengine, vyombo
vya habari vilitaka kupotosha ukweli kwa kuonesha kwamba, Kanisa Katoliki linakumbatia
ushoga. Hati ya Mwisho iliyotolewa na Mababa wa Sinodi baada ya marekebisho ya kina
imeonesha msimamo wa Kanisa unaojikita katika Mafundisho Tanzu na Maandiko Matakatifu.
Askofu
mkuu Kurtz anamsifu na kumpongeza Baba Mtakatifu Francisko kwa kuongoza maadhimisho
ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya familia, kwa kushiriki kikamilifu wakati wote wa
maadhimisho; kwa kusali na kusikiliza kwa makini. Alifungua Sinodi kwa kuwataka wajumbe
kuonesha ujasiri, ukweli na uwazi kadiri watakavyojaliwa na Roho Mtakatifu na kwamba
hata baada ya maadhimisho ya Sinodi, ujumbe wake umeonesha jinsi alivyokuwa kiungo
muhimu katika kuweka mambo sawa!
Kukaa bega kwa bega na Baba Mtakatifu kwa
muda wa majuma mawili, kilikuwa kweli ni kipindi cha neema na baraka kwa Familia ya
Mungu; ameonesha ari na moyo wa huruma na mapendo kwa familia zinazoendelea kuteseka
sehemu mbali mbali za dunia.
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya
Kiswahili ya Radio Vatican.