Kampeni ya kupinga ukatili wa kijinsia nchini Tanzania
TGNP Mtandao ni asasi ya kiraia isiyokuwa na mrengo wa kidini wala kisiasa, iliyoanzishwa
na kusajiliwa zaidi ya miaka 20 iliyopita ikijihusisha na mapambano ya kuleta usawa
wa kijinsia na kuwawezesha wanawake na makundi mengine yalioko pembezoni kwa njia
ya ushawishi na utetezi, machapisho na mafunzo kwa njia mbalimbali kupinga ukatili
wa kijinsia na kuleta mabadiliko ya kijamii kama sehemu ya haki za binadamu.
Pia
TGNP Mtandao hushirikiana na asasi na mashirika mengine ya ndani na nje ya nchi kila
mwaka katika kuadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia.
Licha ya juhudi
mbalimbali za kupambana na ukatili wa kijinsia nchini, bado hali ni mbaya,ambapo takwimu
za wizara ya afya zinaonesha, katika mwaka 2013 asilimia 23% ya wasichana wenye umri
kati ya miaka 15 na 19 walikuwa na mimba au walikuwa na watoto huku zikionesha kuwa
asilimia 18% ya wasichana wa umri huo huolewa utotoni. Takwimu hizo pia zinaonesha
kuwa bado ukeketaji ni tatizo kubwa likiwa bado linatendeka kwa asilimia 15%.
Kauli
mbiu ya kitaifa mwaka 2014 katika kuadhimisha siku hizo ni “Funguka! Fichua Ukatili
kwa maendeleo ya jamii”. Katika kuadhimisha siku hizo, TGNP Mtandao itafanya mjadala
wa wazi utakaoshirikisha zaidi ya watu 500 kutoka katika makundi mbalimbali ya kijamii
wakiwemo wanachi kutoka vituo vya TGNP Mtandao vya taarifa na maarifa kutoka mikoa
mbalimbali nchini Tanzania, makundi yalioko pembezoni, mashirika ya kiraia, wadau
wa maendeleo, wasanii na viongozi wa taasisi mbalimbali za umma.
Aidha kauli
mbiu ambayo imeongoza mjadala huo ni “Siyumbishwi, Najilinda, Mnilinde” unaojikita
kwa vijana hasa wa kike ikiwahimiza wasiyumbishwe, wajiepushe au wajilinde na mambo
au mazingira hatarishi na kuitaka jamii iwajibike kuwalinda na kuwakinga vijana dhidi
ya ukatili wa kijinsia unaotokea katika mazingira mbalimbali nchini Tanzania.