2014-12-01 08:39:48

Hija ya kiekumene ya Papa Francisko nchini Uturuki ilisheheni utajiri mkubwa wa maisha ya kiroho na kiutu!


Padre Federico Lombardi Msemaji mkuu wa Vatican akifanya rejea ya hija ya kiekumene ya Baba Mtakatifu Francisko aliyoihitimisha, Jumapili alasiri anasema kwamba, Baba Mtakatifu aliianza siku yake ya mwisho kwa kukutana na kuzungumza na Bwana Isak Haleva, Rabi mkuu wa Uturuki na baadaye alishiriki kwenye Ibada ya Liturujia Takatifu iliyoongozwa na Patriaki Bartolomeo wa kwanza, kama sehemu ya Maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Andrea, msimamizi wa Kanisa la Costantinopoli.

Ibada hii ilisheheni utajiri mkubwa wa Neno la Mungu uliosindikizwa kwa nyimbo. Neno la Mungu lililosomwa katika Ibada hii ni sehemu ya Injili inayoonesha wito wa Andrea Mtume aliyekutana kwa mara ya kwanza na Yesu, baadaye akamwahabarisha ndugu yake Simoni na tangu wakati huo, wote wawili wakaacha yote na kuanza kuandamana na Yesu katika maisha na utume wake.

Hii imekuwa ni Injili ya Makutano kati ya Yesu na Wafuasi wake, tukio ambalo limeendelezwa na Patriaki Bartolomeo wa kwanza pamoja na Baba Mtakatifu Francisko, ambao kwa pamoja wamekazia umuhimu wa Wakristo kukutana na kutembea kwa pamoja kama ndugu katika Kristo, kama ilivyokuwa kwa Mitume wa Yesu walipokutana na Yesu, wakamwona na kubaki daima pamoja naye katika maisha yao yote.

Liturujia Takatifu ilikuwa na utajiri pamoja na mvuto mkubwa kwa waamini, jambo ambalo limetiliwa mkazo pia na Baba Mtakatifu Francisko kwa kusema kwamba, utajiri wa Neno la Mungu kutoka katika Makanisa mbali mbali ni muhimu sana kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa ndiyo maana Baba Mtakatifu Francisko aliamua kushiriki katika Ibada hii, ili kuonesha utashi wa kiekumene wa kutaka kujenga na kudumisha umoja miongoni mwa Wakristo, siyo tu wakati wa kuadhimisha Fumbo la Ekaristi Takatifu.

Kipaumbele cha kwanza ni kukaa kwa pamoja, ili hatimaye, kuamsha nia ya kuadhimisha Mafumbo ya Kanisa kwa pamoja. Baba Mtakatifu ameshiriki Ibada hii kwa moyo wa uchaji na heshima kubwa, kwani Liturujia Takatifu ni sehemu muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa la Kiorthodox, ndiyo maana, Mapapa wanapotembelea Kanisa la Kiorthodox wanapenda kushiriki katika Liturujia Takatifu, inayoonesha umoja na utofauti hata katika lugha, kama ilivyo hata katika Kanisa Katoliki.

Padre Lombardi anasema kwamba, hotuba zilizotolewa na viongozi hawa wawili zilikuwa na umuhimu wa pekee katika mchakato wa kuendeleza majadiliano ya kiekumene, ili hatimaye, kuweza kufikia umoja kamili miongoni mwa Wakristo. Patriaki Bartolomeo wa kwanza anasema, lengo si kusafisha na kuponya madonda ya utengano yaliyojitokeza katika historia, bali kuangalia mbele kwa imani na matumaini kwani Kanisa Katoliki na Papa wanayo nafasi muhimu sana katika majadiliano ya kiekumene. Khalifa wa Mtakatifu Petro anaonesha ukuu pamoja na dhamana ya upendo na huduma mintarafu mwelekeo wa Kisinodi; mambo msingi katika hija ya kuelekea katika umoja kamili kati ya Wakristo.

Baba Mtakatifu Francisko katika hotuba yake amekazia kwamba, umoja wa Kanisa haulengi kutweza au kuyameza Makanisa, bali kushirikishana karama na utajiri unaofumbatwa katika Makanisa haya, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo, kwani kielelezo cha madaraka ya hali ya juu ndani ya Kanisa kinajionesha katika huduma ya upendo. Makanisa hayana budi kuendelea kushirikiana na kushikamana katika kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu; kuwasaidia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; kudumisha haki, amani na upatanisho kati ya watu; kulinda na kutunza mazingira pamoja na kuwasaidia vijana kupambana kwa ushupavu na changamoto katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Baba Mtakatifu Francisko katika hotuba yake amelaani mauaji ya watu wasiokuwa na hatia yanayofanywa kwa kisingizio cha dini, kama inavyotokea nchini Nigeria, changamoto kwa waamini wa dini mbali mbali kushikamana kwa pamoja kupinga vitendo vya kigaidi vinavyoendelea kusababisha majanga makubwa katika maisha ya watu sehemu mbali mbali za dunia.

Viongozi hawa wakuu wa Makanisa anasema Padre Lombardi, wamekazia umuhimu wa kuendeleza na kudumisha mambo msingi yanayoyaunganisha Makanisa na kwamba, maandalizi ya Mtaguso mkuu wa Makanisa ya Kiorthodox utakaofanyika kunako mwaka 2016 ni hatua muhimu sana katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene, kama Kanisa Katoliki lilivyofanya kwa Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Hili ni tukio la matumaini kwa Makanisa yote.

Viongozi hawa wawili anasema Padre Lombardi wametia sahihi kwenye Tamko la Pamoja na wala hawakusoma, kwani ni mwendelezo wa hija iliyokwishafanywa na Makanisa haya, wakati wa hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Nchi Takatifu, mwezi Mei, 2014. Tamko hili limegusia vita na kinzani za kidini zinazoendelea kujitokeza huko Mashariki ya Kati; umuhimu wa kujenga na kudumisha majadiliano ya kidini na Waamini wa dini ya Kiislam pamoja na mchakato wa ujenzi wa amani nchini Ucrain.

Hii ni kumbu kumbu ya maadhimisho ya Miaka 35 tangu Mtakatifu Yohane Paulo II alipotia sahihi kwenye Tamko la Pamoja kuhusiana na Majadiliano ya Kitaalimungu kati ya Makanisa haya mawili na Patriaki Dimitrios wa kwanza. Tume hii imepewa dhamana ya kujadili na kutafuta ufumbuzi wa changamoto na matatizo yanayokwamisha mchakato wa umoja kamili kati ya Makanisa.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.