Watawa jitahidini kupyaisha maisha yenu kwa ajili ya mchakato wa Uinjilishaji mpya!
Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya amezindua Mwaka wa
Watawa Duniani, uliotangazwa na Baba Mtakatifu Francisko utakaohitimishwa hapo tarehe
2 Februari 2016, kwa kuwataka watawa kufanya tafakari ya kina kuhusu maisha na utume
wao, ili kuweza kushiriki kikamilifu katika mchakato unaopania kupyaisha utume wa
Uinjilishaji, huku wakiendelea kumtumikia Mungu na jirani zao.
Watawa wanatambua
kwamba, mavuno ni mengi, lakini watendakazi katika shamba la Bwana ni wachache na
kwamba, kwa wakati huu Mashirika mengi ya Kitawa na Kazi za Kitume yanakabiliwa na
matatizo pamoja na changamoto mbali mbali za maisha, hasa kutokana na kupungua kwa
idadi ya miito ya maisha ya kitawa, kiasi cha kutia mashaka udumifu wa baadhi ya mashirika.
Kardinali Njue amewataka watawa kuendelea kuwa na matumaini kwani Yesu mwenyewe atawakirimia
yale wanayohitaji kwa ajili ya ujenzi wa Ufalme wa Mungu.
Mama Kanisa anapenda
kutoa fursa hii kwa watawa kufanya tafakari ya kina kuhusu maisha na utume wao na
kuangalia ni kwa jinsi gani wamejitahidi kuwa waaminifu kwa Mungu na Kanisa hasa kwa
kuzingatia Nadhiri zao, ili kuanza tena upya kwa kishindo na mwamko mkuu. Uinjilishaji
wa kina unahitaji watu wanaojisadaka bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani.
Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya katika Mwaka wa Watawa Duniani litaandaa semina
na kozi mbali mbali zitakazowasaidia watawa kutekeleza dhamana na wajibu wao kikamilifu.
Naye
Askofu mkuu Charles D. Balvo, Balozi wa Vatican nchini Kenya amewapongeza watawa kwa
utume wao katika mchakato wa Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima:
kiroho na kimwili. Ameona na kushuhudia majitoleo ya watawa katika maisha na utume
wa Kanisa hasa miongoni mwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii.
Katika
utume wake kama Balozi wa Vatican nchini Kenya na Sudan ya Kusini ameonja sadaka kubwa
inayotolewa na watawa kwa ajili ya Mungu na kuwashukuru na kwamba, umefika wakati
wa kufanya tafakari ya kina, ili kuangalia jinsi ambavyo wanaweza kujisadaka zaidi,
kwa kumwilisha karama ya Mashirika yao kati ya watu wanaowahudumia pamoja na kuendelea
kuwa waaminifu kwa Mungu na kwa Kanisa.
Uzinduzi wa Mwaka wa Watawa Dunini
huko Kenya, umehudhuriwa na viongozi mbali mbali kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki
Kenya pamoja na watawa kutoka katika Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume. Kauli
mbiu inayoongoza maadhimisho haya ni "Watawa amkeni ili kuwaamsha walimwengu".